• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 8:27 PM
Umuhimu wa mazingira mazuri kwa watahiniwa

Umuhimu wa mazingira mazuri kwa watahiniwa

Na SAMMY WAWERU

MAANDALIZI ya mitihani ya kitaifa ya elimu ya msingi KCPE na sekondari KCSE yanaendelea kote nchini.

Jumatatu, Waziri wa Elimu Prof George Magoha alisema kila kitu kiko shwari linapokuja suala la mitihani hiyo inayotarajiwa kuanza baada ya wiki mbili zijazo.

Ule wa darasa la nane, KCPE utaanza Oktoba 28 na kukamilika Oktoba 31.

Nao wa kidato cha nne, KCSE unatarajiwa kuanza Novemba 4 na kutia nanga Novemba 27.

Akizungumza katika Taasisi ya Mafunzo ya Serikali (KSG), Waziri Magoha alihakikishia taifa kuwa hakutakuwa na visa vyovyote vya udanganyifu wa mitihani wala ufichuzi.

“Hakutakuwa na mtihani utakaofunguliwa kabla ya asubuhi ya siku ya siku,” alisema.

Hata hivyo, Prof Magoha alisema kuna baadhi ya ‘wahuni’ wenye nia ya kutekeleza udanganyifu wakati wa shughuli hiyo ya kitaifa na alionya kuwa serikali itawachukulia hatua kali kisheria.

Wizara ya Elimu, Usalama wa Ndani na Mawasiliano na Teknolojia (ICT) zitashirikiana kufanikisha shughuli hizo za kitaifa.

Walimu 180,000 wameteuliwa kulifanikisha. Pia, kuna helikopta kadhaa zilizotengewa shughuli hiyo hususan kwa maeneo yenye ubovu wa barabara na kushuhudia utovu wa usalama.

Mbali na wizara ya elimu, asasi zingine husika ni baraza la kitaifa la mitihani (Knec) na tume ya waajiri walimu nchini, Tsc.

Wakati serikali inajifunga kibwebwe kuandaa shughuli hiyo ya kitaifa, watahiniwa wanaendelea kubukua vitabu. Kila sekunde, dakika na saa inapoyoyoma, wanahakikisha wanajikumbusha waliyopokea darasani, kuanzia darasa la kwanza hadi nane.

Bi Muriuki Wanjugu, ambaye ni mwalimu mkuu wa shule binafsi ya Kiangai Blessings View Academy iliyoko Kaunti ya Kirinyaga anasema katika muda wa lala salama, wanafunzi wanapaswa kuwa na ukuruba na mlahaka mzuri na walimu.

“Asijalishwe na iwapo ni mwalimu wa somo lake au la, kila mwalimu aliye shuleni anamosomea amfanye rafikiye wa karibu na kuuliza maswali,” anashauri Wanjugu.

Kulingana na mwalimu huyo kipindi hiki kisiwe cha kujipa presha, ila kiwe cha kujikumbusha aliyosoma mtahiniwa awali na kujua mapya ambayo pengine hakuyawahi.

“Ninahimiza walimu pia wawapokee wanafunzi wanaofanya mitihani na wajitolee kuwaandaa sambamba,” anaeleza mwalimu huyo, akishauri kwamba huu ni muda wa kutumia karatasi za mitihani ya kitaifa iliyopita ili kujua muundo wa maswali.

Kujadiliana

Isitoshe, watahiniwa wanatakiwa kuwa katika makundi ya kujadili maswali na masomo mbalimbali, kinachowalemea waalike mwalimu au walimu kuwatatulia.

“Makundi yatawawezesha kubadilishana mawazo na hata maarifa,” anasisitiza mwalimu Pauline Nyaguthii, wa Kiambu.

Kwa upande wao wazazi wanapaswa kujua kuwa huu si wakati wa kuwapa watahiniwa majukumu ya kinyumbani, kama vile kuosha vifaa vya kula, nguo na kuwaagiza kuenda shambani. Wanahimizwa kushirikiana nao kuhakikisha wanapata muda wa kutosha kudurusu vitabu na hata kupumzika.

“Kipindi hiki wanafunzi wanaofanya mitihani ya kitaifa kama wazazi tunapaswa kuwapenda zaidi na kuwaepusha na kazi za nyumbani,” anasema Elizabeth Wakaguyu ambaye ni mzazi wa mtahiniwa anayetarajiwa kufanya KCPE 2019.

Kiwewe wanachoshuhudia watahiniwa chini ya mfumo wa zamani wa 8-4 – 4 hususan wakati wa mitihani ya kitaifa, huenda kikafikia kikomo mfumo mpya wa CBC ukitekelezwa kikamilifu.

Aidha, CBC ni mfumo unaojiegemeza zaidi katika uamilifu na kukuza vipaji vya wanafunzi badala ya kuwatathmini kupitia mitihani ambayo ni maswali ya yaliyofundishwa darasani.

You can share this post!

Pasta ajuta kuvuruga wapenzi

UKUMBI WA LUGHA NA FASIHI: Aibu ya mapenzi

adminleo