• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
KAULI YA MATUNDURA: Tajiriba za waandishi kuhusiana na sera ya kudhibiti fasihi ulimwenguni – 4

KAULI YA MATUNDURA: Tajiriba za waandishi kuhusiana na sera ya kudhibiti fasihi ulimwenguni – 4

Na BITUGI MATUNDURA

HII ni awamu ya nne ya makala kuhusu sera ya udhibiti wa maandishi kwa waandishi wa fasihi ulimwenguni.

Juma lililopita, nilitaja kwamba Ngugi wa Thiong’o ni mmoja wa watunzi waliofarakana na mamlaka na vyombo vyao vya dola kutokana na sera hii.

Aidha niliangazia maoni ya wakili Issa Shivji wa Tanzania kuhusu jukumu la waandishi, wasomi na wanaharakati katika jamii. Shivji anadai kwamba waandishi wana nafasi muhimu katika mapambano ya kiukombozi. Hata hivyo, isichukuliwe kwamba Ngugi na Euphrase Kezilahabi ndio watunzi pekee ambao kazi zao zimewahi kukabiliwa na udhibiti.

Tuna waandishi wengine kama vile David Maillu ambaye kazi zake pendwa kama vile Unfit for Human Consuption, After 4.30, na My Dear Bottle zilikabiliwa na udhibiti. Nje ya Afrika ya Mashariki, tuna mwandishi Sir Ahmed Salman Rushdie ambaye aliandika Satanic Versers.

Kazi hii ambayo imetumia kiunzi cha maisha ya Mtume Muhammad (SAW) ilipochapishwa nchini Uingereza mnamo 1988, Waislamu wengi walimshutumu Salman Rushdie kwa madai ya kukufuru. Mnamo 1989, kiongozi wa Iran Ayatollah Ruhollah Khomeini alitoa amri ya fatwa kuwataka Waislamu wamuue Rushie.

Mauaji kadha, majaribio kadha ya mauaji na mashambulizi kwa mabomu vilitokea kwa minajili ya kuipinga riwaya hiyo. Serikali ya Iran iliunga mkono fatwa hiyo hadi 1998 wakati serikali iliyoshika hatamu ya rais Mohammad Khatam iliposema kwamba haikuwa inaunga mkono tena suala la kumuua Rushdie.

Masaibu yaliyomkabili Salman Rushdie yanatokana na udhibiti wa maandishi unaotekelezwa na asasi za kidini. Mfasiri wa kazi hiyo kwa lugha ya Kijapani aliuawa kwa kudungwa kisu mjini Tokyo, huku mchapishaji wake nchini Norway akiuawa kwa kupigwa risasi mjini Oslo.

Aidha, mfasiri wa kazi hiyo kwa lugha ya Kiitaliano vilevile aliuawa kwa kudungwa kisu na umati wa watu waliokuwa wakitaka awaeleza alikokuwa amejificha Salman Rushdie.

Nchini Bangladesh, mwandishi wa kike Taslima Nasrin – mshairi na mwanariwaya alilazimika kwenda mafichoni mnamo 1993 baada ya kuaibishwa na kudhulumiwa hadharani (alipigwa na kuvuliwa nguo) na kuandamwa kwa kuandikia masuala ‘yasiyoruhusiwa’ kama vile ‘ubakaji katika ndoa’.

Riwaya yake, Lajja (Aibu) ilipigwa marufuku. Nchi nyingine ulimwenguni ambazo zimewahi kuwafunga waandishi gerezani ni China, Burma, Korea Kusini, Syria na Vietnam. Mwandishi na mshairi wa Malawi, Jack Mapanje alifungwa gerezani mnamo 1987 kwa kuandika mkusanyo wa mashairi Of Chameleons and Gods ambao uliikosoa serikali ya Hastings Banda.

Nchini Nigeria, mwandishi maarufu Ken Sawo Wiwa aliyeandika A Month and a Day: A Detention Diary aliuawa na wanajeshi katika utawala wa Sani Abacha kwa kutetea watu wa jamii yake ya Ogoni dhidi ya dhuluma za kupunjwa na kampuni za kimataifa zilizokuwa zinajishughulisha na uchimbuaji wa mafuta.

Mwandishi mwingine kutoka nchi hiyo, Wole Soyinka alikimbilia uhamishoni nchini Marekani mnamo 1994.

Tajiriba ya Salman Rushdie kufuatia kuchapishwa kwa riwaya yake ya Satanic Verses na waandishi wengine ambao nimekwisha kuwataja zinaakisi mwengo wa masaibu yaliyowahi kumkumba Ngugi wa Thiong’o chini wa utawala wa serikali za Jomo Kenyatta na Daniel Arap Moi.

Ngugi wa Thiong’o anaandika: “Ninafahamishwa, kwa mfano, kwamba mnamo Desemba 1977 watu wawili wenye mamlaka makuu serikalini waliabiri ndege hadi Mombasa na kutaka wakutane kwa dharura na Jomo Kenyatta. Kila mmoja alikuwa na nakala ya vitabu vyangu, Petals of Bloood na Ngahika Ndeenda. Ombi lao lilipokubaliwa, walimsomea Jomo Kenyatta, bila shaka nje ya muktadha, vifungu na sentensi na maneno waliyofasiri kwamba nilikuwa na njama ya kutekeleza maovu.”

 

[email protected]

You can share this post!

KINA CHA FIKIRA: Iweje wageni wanakifurahia Kiswahili huku...

MAPITIO YA TUNGO: Pepo za Mizimu; Novela faridi kuhusu...

adminleo