• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 3:03 PM
OBARA: ICC ikome kutonesha vidonda vya wahanga wa fujo 2007

OBARA: ICC ikome kutonesha vidonda vya wahanga wa fujo 2007

Na VALENTINE OBARA

MAJIBIZANO kuhusu kesi za ghasia zilizotokea baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2007 ni kama kukejeli waathiriwa wa ghasia hizo.

Kila mwaka Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) hutoa ripoti ya shughuli zake ambapo mojawapo ya masuala yanayogusiwa ni kuhusu kesi hizo, ambazo zote zilisitishwa kwa sababu mbalimbali.

Ripoti hizo kutoka kwa kitengo cha kuendesha mashtaka ambacho kinasimamiwa na Bi Fatou Bensouda huwa hazituelezi chochote kipya ila kurudia mambo yale yale tunayofahamu.

Hayo ni kama vile kwamba, kesi zilifeli kwa ssbabu ya mashahidi kuhongwa, kutishiwa au kuuawa, na vile vile ukosefu wa ushirikiano kutoka kwa serikali ya Kenya kukusanya ushahidi muhimu uliohitajika.

Wiki iliyopita, kitengo hicho kilitoa ripoti ya kina ijapokuwa si kamili ya uchunguzi uliofanywa na wataalamu wa sheria za haki za kibinadamu kimataifa kuhusu kilichosababisha kesi hizo kusitishwa.

Kando na mambo ya kawaida tuliyoyazoea, kulionekana pia hali ya kulaumiana kati ya wasimamizi wa sasa wa idara ya kuendesha mashtaka, na wale waliotangulia wakiongozwa na Bw Louis Moreno-Ocampo.

Hii haikuwa mara ya kwanza Bw Ocampo kulaumiwa kwa usimamizi mbaya wakati wa ukusanyaji ushahidi ambao ungetegemewa katika kesi za washukiwa wakuu waliojumuisha Rais Uhuru Kenyatta na naibu wake, Dkt William Ruto.

Vijisababu hivi vinavyotolewa na ICC pamoja na lawama hazisaidii kivyovyote kumletea haki Mkenya mlala hoi ambaye alipoteza mali yake, akajeruhiwa kwa kiasi cha kuwa mlemavu daima, na yule ambaye alipoteza wapendwa wake kwa ukatili uliofanywa na majambazi na polisi waliotegemewa kulinda raia.

Matukio ya kutisha tuliyoshuhudia mwishoni mwa mwaka wa 2007 hadi mwanzoni mwa 2008 si jambo la kufanyia mzaha.

Inachukiza mno ikiwa kila mara tutakuwa tukiona matukio hayo yakitumiwa tu kama msingi wa kufanya utafiti au wa watu kujitafutia ubabe katika nyanja tofauti ilhali bado kuna maelfu ya waathiriwa ambao hawajatendewa haki hadi sasa.

Waathiriwa wengi walipewa matumaini ya kupokea haki katika ICC kwani inavyoonekana, serikali haijajitolea kikamilifu hadi sasa kuchukua hatua dhidi ya wahusika wa ghasia hizo wala kulipa ridhaa ya kutosha kwa waliopata hasara.

Inafahamika kwamba kesi zilizopelekwa ICC zingali wazi kufunguliwa upya ikiwa ushahidi mpya unaoweza kutegemewa utapatikana katika siku za usoni.

Kile ambacho waathiriwa pamoja na watetezi wa haki walio na utu wanataka kujua ni kama wanafaa kuendelea kuwa na matumaini ya kupata haki, au wakubali hatima yao ya kuishi kwa athari zilizowakumba milele.

Itakuwa busara kama kitengo cha kuendesha mashtaka katika mahakama hiyo ya kimataifa itakoma kuwapa waathiriwa matumaini bila nia ya kutenda lolote jipya kwani ripoti hizi zinazotolewa mara kwa mara zinaibua kumbukumbu tusizipenda.

You can share this post!

WASONGA: Viongozi waendeshe kampeni ya kupanda miti

BBI: Macho yote sasa kwa Ruto

adminleo