• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
KAULI YA MATUNDURA: Athari ya sera ya udhibiti kwa waandishi wa fasihi ulimwenguni – Sehemu ya tano

KAULI YA MATUNDURA: Athari ya sera ya udhibiti kwa waandishi wa fasihi ulimwenguni – Sehemu ya tano

Na BITUGI MATUNDURA

HII ni awamu ya tano ya msururu wa makala yangu kuhusu athari ya sera ya udhibiti kwa waandishi wa fasihi.

Mawazo haya yanatokana na makala niliyowasilisha katika kongamano ya kimataifa la Chama cha Kiswahili cha Afrika ya Madharihi – CHAKAMA katika Chuo Kikuu cha Maasai Mara mnamo Novemba.

Kutokana na makala yaliyopita, imebainika kuwa motifu ya masaibu yaliyomkumba Ngugi wa Thiong’o inajitokeza pia tunapomchunguza mwandishi Abdilatif Abdalla.

Mshairi huyu anayefahamika sana kwa diwani yake ya ushairi ijulikanayo kama ‘Sauti ya Dhiki’ (Oxford University Press, 1973) aliyoitunga akiwa kifungoni tangu Machi 1969 mpaka Machi 1972.

Abdilatif anasema: “Ingawa hapa si mahali pa kueleza sababu ya mimi kufungwa, naona ni dharura niitaje kwa vile ambavyo pengine nisingeyatunga mashairi haya kama nisingekuwa nimefungwa. Sababu ya kufungwa ni kwamba nilipatikana na “hatia ya kuchochea watu kuipindua Serikali ya Kenya kwa kutumia silaha” baada ya kuandika, kuchapisha na kuisambaza kwenye miji kadha wa kadha ya Jimbo la Pwani la Kenya karatasi niliyoiita Kenya: Twendapi?”

Mwandishi mwingine ambaye tajriba zake zinakurubiana na za Ngugi wa Thiong’o na Abdilatif Abdalla ni Katama Mkangi. Mkangi alikuwa mkosoaji mkubwa sana wa serikali ya Moi. Alikuwa ni mmoja wa watu waliopigania sana demokrasia nchini Kenya mnamo miaka ya 1980.

Kutokana na misimamo na maoni yake, Mkangi alikamatwa mnamo Machi 5, 1986 kwa madai ya kuwa mwanachama wa kundi la Mwakenya, na kuwekwa kizuizini kwa miaka miwili. Wasomi wengine waliokamatwa pamoja naye kipindi hicho ni pamoja na Profesa Isaiah Ngotho Kariuki na Maina wa Kinyatti.

Baada ya kuondoka kizuizini, Mkangi alikaa kwa muda mrefu bila ajira kwa sababu hangeweza kurudi katika chuo kikuu kufundisha kwa sababu ya kubandikwa ‘mwasi’.

Akionesha muumano na mfanano wa kimawazo na kiitikadi uliopo baina ya Ngugi wa Thiong’o na Abdilatif Abdalla Kresse (2016) anasema: Hiki ni kiungo kati ya Abdalla rafiki na mshirika wake Ngugi wa Thiong’o, ambaye mara nyingi anamwona Abadalla kama kielelezo chema katika ukosoaji wa kisiasa na mwandishi mahiri wa fasihi ya Kiafrika, asiyetetereka katika kuuliza maswali muhimu ambayo yanapaswa kujibiwa.

Wawili hao kwa hakika wanaweza kulinganishwa kwa misingi ya kujitolea kwao kimaadili na katika mapambano ya kisiasa katika nchi yao, na imani yao kwamba nyenzo yoyote ile ya kujieleza kimaandishi – ikiwemo karatasi/makala ni njia ya kutumika katika mapambano hayo.

Wote waliendeleza juhudi hizi wakiwa wangali uhamishoni London (na kwingineko), katika kupinga serikali ya Moi. Tunakubaliana na maoni haya kwa misingi kwamba kuna uwezekano mkubwa wa waandishi walioandika katika kipindi sawa na mazingira sawa kuwa na mwitiko sawa kuihusu jamii yao.

Kitovu kinachowaunganisha Ngugi wa Thiong’o na Abdilatif Abdalla mbali na itikadi yao ya kuegemea Umaksi ni utawala wa Moi ambao watunzi hawa hawakukubaliana nao.

Mhakiki, Mwenda Mbatiah anasema: Ngugi na Mkangi ni waandishi maarufu ambao kazi zao husomwa kote Afrika Mashariki na kwingineko. Watunzi hawa pia ni wasomi, ingawa ni wataalamu katika nyanja tofauti.

Ngugi ni mwanafasihi, mhakiki na mwandishi huku Mkangi akiwa ni mwanasosholojia. Hata hivyo, watunzi hawa huandika kazi zinazosawiri dhiki za umma, ndoto na matamanio yao.

Muhimu zaidi ni kwamba, watunzi hawa wana itikadi sawa ya kisiasa ambayo inaegemea sana Umaksi. Wote wawili walikamatwa na kuwekwa kizuizini. Ingawa waliachiliwa huru hatimaye, hawakuruhusiwa kurejea kufundisha katika Chuo Kikuu cha Nairobi.

 

[email protected]

You can share this post!

KINA CHA FIKIRA: Raha iliyoje Kiswahili kufundishwa rasmi...

NDIVYO SIVYO: Mvua ikipungua huwa ‘imepusa’ na...

adminleo