• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 7:50 AM
Maimamu wataka tume mpya ibuniwe kusaidia EACC

Maimamu wataka tume mpya ibuniwe kusaidia EACC

Na TITUS OMINDE

BARAZA la Maimamu na Wahubiri wa Kenya (CIPK) ukanda wa North Rift linataka serikali kuunda tume mpya ya kusaidia Tume ya Kukabili Ufisadi (EACC) ambayo baraza hilo linadia imelemewa kutekeleza majukumu yake.

Mwenyekiti wa CIPK Sheikh Abubakar Bin alisema kuna haja ya kubuniwa kwa tume mbadala ili kuboresha utendakazi wa EACC.

Sheikh Bin alisema EACC imeshindwa kupiga msasa Wakenya wasiokuwa na maadili kabla ya kuruhusiwa kugombea nyadhifa mbalimbali katika afisi za umma.

Alitolea mfano kuidhinishwa kwa gavana wa Nairobi Mike Sonko ambaye kwa mujibu wao ameshindwa ecckuonyesha uadilifu wa uongozi.

Akihutubu mjini Eldoret, Sheikh Bin alisema kesi ya sasa ya ufisadi inayomkabili gavana huyo ni dalili dhahiri za kutofaulu kwa EACC katika jukumu lao la kuwachunguza wanasiasa kabla ya kuwaidhinisha kugombea viti husika.

Alipendekeza viongozi wa dini wapewe jukumu la kutoa vyeti vya maadili kwa Wakenya wanaopania kugombea nyadhifa serikalini.

“Viongozi wa dini wanapaswa kupewa jukumu la kuchunguza viongozi wanaokusudia kuteuliwa katika ofisi za umma,” alisema Bin

Kiongozi huyo wa CIPK alijuta kwamba kwa sababu za ukosefu wa uwazi na uadilifu wa viongozi wengi nchini kumechangia ufisadi na ukosefu wa maadili unaozidi kuwa kero kila uchao.

Akirejelea tabia ya gavana Sonko alipokuwa akikamatwa na maafisa wa polisi eneo la Voi wiki iliyopita, alisema tabia hiyo inaashiria ukosefu wa maadili.

“Mfano ambao gavana Sonko alionyesha wakati alipokamatwa na maafisa wakuu wa polisi huko Voi ulionyesha wazi kuwa yeye si kiongozi mwenye maadili. EACC na DCI lazima wawajibikie tabia hiyo potovu,” alisema Sheikh Bin.

You can share this post!

Korti kuamua iwapo Rais atashurutishwa kuwaapisha

Juhudi za kuzima ‘muguka’ zafeli

adminleo