• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 3:23 PM
MWANASIASA NGANGARI: Mzee Moi: Mlezi wa vigogo wa kisiasa nchini Kenya

MWANASIASA NGANGARI: Mzee Moi: Mlezi wa vigogo wa kisiasa nchini Kenya

Na KEYB

ALIPOKUWA akichunga mifugo wa familia katika kijiji cha Kurieng’wo, Sacho, Kaunti ya Baringo, hakuna aliyedhani kuwa siku moja Daniel Toroitich Arap Moi angekuwa mwalimu, mwanasaisa na Rais wa Kenya.

Kijana aliyekuwa akichunga mifugo alitawala Kenya kwa miaka 24 kuanzia 1978 hadi 2002 na kulea wanasiasa na viongozi wa sasa na pengine watakaotawala nchi hii siku nyingi zijazo.

Moi mwenye umri wa miaka 95, alizaliwa Septemba 2, 1924, katika kijiji cha Kurieng’wo, Sacho, wilayani Baringo akiwa mwana wa tano wa mke wa kwanza wa baba yake.

Kama jina Jina lake Toroitich, linavyomaanisha “karibisha mifugo nyumbani” Moi alianza kuchunga mifugo kama vijana wengine wa jamii yake katika kijiji chao.

Baba ya Moi alikufa akiwa na umri wa miaka minne na kaka yake, Tuitoek, akawa mlezi. Ni Tuitoek aliyemshawishi Moi kwenda shule akiwa na umri mdogo ili aweze kutoroka umasikini na dhuluma za kikoloni.

Mnamo 1934, Moi alianza masomo katika shule ya Africa Inland Mission, Kabartonjo, takribani kilomita 45 kutoka nyumbani kwao.

Mnamo Oktoba 20, 1936, alibatizwa na kuitwa Daniel. Mwaka wa 1938, alihamishiwa shule ya African Inland Mission, Kapsabet na baadaye shule ya African School Kapsabet, ambapo alikuwa kiranja mkuu na nahodha wa timu ya soka. Alifanya kazi za vibarua akiwa shuleni na nje ya shule ili aweze kukimu mahitaji yake ya kimsingi.

Mnamo 1945, Moi alichaguliwa kujiunga na shule ya upili ya Alliance lakini, kwa masikitiko, serikali ya kikoloni haikumruhusu. Badala yake, alitumwa chuo cha mafunzo ya ualimu. Maswali yamekuwa yakiulizwa: Kwa nini serikali ya kikoloni ilimnyima Moi nafasi muhimu ya kusomea Alliance? Ni nini walikuwa wameona ndani yake?

Alipomaliza mafunzo ya ualimu, alitumwa Kabarnet kama mwalimu mkuu. Alisoma binafsi na kufuzu mtihani kwa London Matriculation Examinations. Mnamo 1949, alipandishwa cheo na kuwa mwalimu wa kiwango cha P2 baada ya kozi fupi katika chuo cha Kagumo.

Alihamishwa hadi Tambach Government African School kama mwalimu wa walimu. Moi alimuoa Helena (Lena) Bomet mwaka wa 1950 na wamejaliwa watoto wanane- mabinti watatu na wavulana watano.

Mnamo 1950 alihudhuria mafunzo katika Jeans School (sasa inajulikana Kenya School Of Goverment) na baadaye akatumwa kufanya kazi Government African School, Kabarnet, ambako alifunza hadi 1955 alipojiunga na siasa.

Kujiunga na siasa kwa Moi, kulifuatia mkutano aliofanya na kundi la wapiganaji wa uhuru chini ya uongozi wa Brigedia Daniel Njuguna aliyemtembelea Juni, 1955. Aliunga vita vyao na baada ya kuwalisha na kuwakinga kwa wiki mbili, aliwapatia chakula na Sh500.

Mnamo Oktoba 1955, Moi alichaguliwa kutoka orodha ya watu wanane walioteuliwa kujaza nafasi iliyoachwa wazi na Joseph ole Tameno, ambaye alikuwa amejiuzulu kutoka kiti kisichokuwa rasmi katika Legco.

Moi alipoketi Legco akiwa na wanachama wengine wanne pekee Waafrika mnamo Oktoba 18, 1955, hakujua yaliyokuwa yakimsubiri katika siasa.

Hata hivyo, alikabiliana na changamoto mpya na, mnamo 1956, aliwasilisha mswada kutaka walimu Waafrika, waruhusiwe kuunda chama chao wenyewe.

Chama cha Kitaifa cha Muungano wa Walimu Kenya (Knut) kiliundwa na kusajiliwa was 1957. Alishirikiana na viongozi wengine kama vile Eliud Mathu, Ronald Ngala na Masinde Muliro, kutetea Jomo Kenyatta kuachiliwa kutoka kizuizini na idadi ya Waafrika katika Legco kuongezwa. Mnamo 1959, aliongoza kundi la viongozi kumtembelea Kenyatta kizuizini Lodwar.

Mnamo 1960, Moi na wanachama wengine Waafrika katika Legco, walishiriki katika mazungumzo ya kikatiba katika Lancaster House jijini London katika maandalizi ya Uhuru wa Kenya kutoka kwa Uingereza.

Waliporudi nchini, walinuia kuanzisha chama kimoja cha kitaifa cha kisiasa. Lakini tofauti kati yao zilifanya waunde vyama viwili- Kanu cha Gichuru, Odinga na Mboya kilichobuniwa Kiambu, na Kadu cha Ngala (Rais au kiongozi wa chama), Moi (mwenyekiti), Muliro (naibu mwenyekiti) na Martin Shikuku (katibu mkuu) walichounda wakiwa Ngong.

Moi na wengine katika Kadu, ambao walitoka jamii ndogo, walikataa Kanu wakidai ilikuwa ikiwakilisha maslahi ya jamii kubwa, Waluo na Wakikuyu. Kwa hivyo, waliamua kuunda muungano wa makabila mengi.

Kwenye uchaguzi wa 1961, Kanu ilishinda viti 19 na kikapata Kadu 11. Lakini Kanu ilikataa kuunda serikali hadi Kenyatta aachiliwe huru. Lakini Kadu ilikubali na Moi akateuliwa Katibu wa Bunge(waziri msaidizi) katika Wizara ya Elimu mnamo 1961. Baadaye alihudumu katika wizara za Elimu na Serikali za Wilaya.

Katika uchaguzi wa 1963 ambao ulileta uhuru, Kadu ilikataa kuwasilisha wagombeaji kupinga Kanu, kilichokuwa wakati huo chini ya uongozi wa Kenyatta baada ya kuachiliwa kutoka kizuizini 1961. Kadu kilishindwa na kuwa katika Upinzani. Kenyatta alichaguliwa Waziri Mkuu.

Akiwa mwenyekiti wa Kadu, Moi aliona utata wa siasa na akaamua kufuata mfumo wa umoja wa kitaifa. Hii ndiyo ilifanya Kadu kuvunjwa Novemba , 1964. Wanachama walijiunga na Kanu na Kenya ikawa taifa ya chama kimoja, japo sio kisheria.

Kenyatta alimteua Moi Waziri wa Mashauri ya Ndani, wadhifa ambao alihifadhi hata alipokuwa Makamu wa Rais. Mashauri ya Ndani ulikuwa wadhifa muhimu kwa sababu alikuwa akisimamia magereza, polisi na Idara ya Uhamiaji.

Kulingana na Toleo la Africa Confidential la Juni, 1990, lilisema Moi alitumia Wizara ya Mashauri ya Nyumbani kufanya urafiki na watu wengi kote nchini ambao ulimfaa miaka ya baadaye.

Jukumu lake la kutoa paspoti lilimkutanisha na wafanyabiashara kutoka bara Asia na makampuni kutoka Uingereza.

Lilikuwa jukumu la Moi pia, kuteua wakuu wa polisi, magereza na huduma za uhamiaji. Hii ilimfaidi miaka ya baadaye wakati huduma ya polisi ilikuwa imejaaa watu ambao Moi aliteua.|

Lakini kumezwa kwa Kadu hakukutuliza siasa. Badala yake, kulizua vita chungu katika Kanu asilia, kati ya mirengo miwili, mmoja ukimuunga Rais Kenyatta na mwingine Makamu- Rais Odinga.

Kufikia 1966, tofauti zilikuwa zimefikia kiwango ambacho hazingetatuliwa na wakati Odinga alipovuliwa wadhifa wa makamu wa rais katika kongamano la Limuru, alijiuzulu kutoka chama hicho na kuunda KPU.

Joseph Murumbi, aliyekuwa Waziri, aliteuliwa Makamu- Rais. Lakini hakajiuzulu hata kabla ya kumaliza mwaka. Mnamo Januari, 1967, aliteuliwa makamu wa rais wa tatu wa Kenya akiwa na umri wa miaka 43.

Wadadisi wanasema kwamba Kenyatta alimteua Moi kwa sababu hakuwa ameunga mrengo wowote katika vuta nikuvute za kisiasa kati ya Wakikuyu na Wajaluo. Hata hivyo, katika kitabu chake , Not yet Uhuru, Oginga alisema Moi alikuwa sawa na twiga mwenye shingo ndefu anayeona mbali.

Kati ya 1970 na 1978, kulikuwa na shinikizo apokonywe wadhifa wa makamu wa rais ili asiweze kumrithi Mzee Kenyatta moja kwa moja kwa mjibu wa katiba. Waliokuwa karibu na Mzee Kenyatta walitaka katiba ifanyiwe mageuzi ili makamu wa rais asiwe akimrithi rais akifa akiwa mamlakani kwa siku 90.

Alihudumu kama makamu rais kwa miaka 11 na Kenyatta alipokufa Agosti 22 1978, alisaidiwa na viongozi wa jamii ya Wakikuyu kama vile Mwai Kibaki ambaye wakati huo alikuwa waziri wa fedha na Charles Njonjo aliyekuwa Mkuu wa sheria kuingia mamlakani na kutoka wakati huo alitawala Kenya kwa miaka 24.

 

Kwa hisani ya Kenya Yearbook Editorial Board; kenyayearbook.co.ke

You can share this post!

Mshtuko kwa wazazi baada ya karo kupanda

KINAYA: ‘Ouru’ ajitokeze kimasomaso na kueleza...

adminleo