• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 1:47 PM
GOLD COAST AUSTRALIA: Unyonge wa Wakenya mbio za masafa mafupi

GOLD COAST AUSTRALIA: Unyonge wa Wakenya mbio za masafa mafupi

Na CHRIS ADUNGO

NDOTO za Kenya za kutia fora katika mbio za masafa mafupi kwenye makala ya 21 ya Michezo ya Jumuiya ya Madola zilizimika kabisa hapo Jumatano baada ya wanariadha waliokuwa wakipeperusha bendera ya taifa hili kutotamba katika fani hizo.

Mark Otieno Odhiambo na Millicent Ndoro walibanduliwa kwenye nusu-fainali za mbio za mita 200 kwa upande wa wanaume na wanawake mtawalia huku Maximila Imali akikamilisha mbio za mita 400 kwa muda wa sekunde 51.32 uliomweka katika nafasi ya tano nyuma ya Christine Botlogetswe wa Botswana (sekunde 51.17).

Mtimkaji Stephenie Mcpherson wa Jamaica aliridhika na nishani ya shaba katika mbio hizo baada ya kuambulia nafasi ya tatu kwa muda wa sekunde 50.93 nyuma ya mwenzake wa Jamaica, Anastasia Le-Roy aliyejinyakulia medali na fedha kwa kufikia ukingo baada ya sekunde 50.57.

Nyota wa Botswana, Amantle Montsho, ndiye aliyejizolea nishani ya dhahabu baada ya kuzitawala mbio hizo kwa sekunde 50.15. Mgongo wa Imali alifuzu kwa fainali ya jana baada ya kutawala kundi la pili kwenye nusu-fainali ya mbio hizo kwa sekunde 51.52, mbele ya mwanariadha mzawa wa Nigeria, Yinka Ajayi aliyevuta mkia katika fainali ya jana (52.26).

Ajayi alisalia kusoma migongo ya Anneliese Rubie (sekunde 52.03, Australia) na Hima Das (sekunde 51.32, India).

You can share this post!

GOLD COAST AUSTRALIA: Wanaotegemewa na Kenya mita 800 kwa...

GOLD COAST AUSTRALIA: Ni shaba tu kwa bondia Christine

adminleo