• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 5:55 AM
Shujaa kumenyana na Tonga Kombe la Dunia

Shujaa kumenyana na Tonga Kombe la Dunia

Na GEOFFREY ANENE

DROO ya Kombe la Dunia ya raga ya wachezaji saba kila upande imefanywa, huku Shujaa ya Kenya ikikutanishwa na kisiwa cha Tonga katika mechi yake ya ufunguzi mnamo Julai 20, 2018 mjini San Francisco, Marekani.

Vijana wa kocha Innocent Simiyu hawakupata tiketi ya moja kwa moja ya raundi ya 16-bora baada ya kumaliza katika nafasi ya tisa katika orodha ya matokeo ya Raga ya Dunia ya msimu 2016-2017 na 2017-2018 hapo Aprili 11.

Mshindi kati ya Kenya na Tonga atakutana na Scotland katika raundi ya 16-bora.

Afrika Kusini, Fiji, New Zealand, Uingereza, Marekani, Australia, Argentina na Scotland zilipata tiketi za bwerere kushiriki mechi za raundi ya 16-bora baada ya kumaliza misimu hiyo miwili ya Raga ya Dunia (hadi duru ya Hong Kong Sevens mwaka 2018) katika nafasi nane za kwanza, mtawalia.

Mshindi kati ya Canada na Jamaica atalimana na Argentina, Australia inasubiri mshindi kati ya Ufaransa na Papua New Guinea, nazo Wales na Zimbabwe zitapigania tiketi ya kukutana na Marekani.

Atakayeibuka mshindi kati ya Samoa na Hong Kong atavaana na Uingereza, nayo New Zealand itapambana na mshindi kati ya Urusi na Uganda, ambayo inanolewa na Mkenya Tolbert Onyango.

Japan na Uruguay zitapigania tiketi ya kumenyana na Fiji nayo Jamhuri ya Ireland itakabana koo na Chile kupata tiketi ya kushindania nafasi ya kuingia robo-fainali dhidi ya Afrika Kusini.

Kenya ilifika nusu-fainali ya makala mawili yaliyopita. Ilimaliza katika nafasi ya tatu mwaka 2009 nchini Urusi nyuma ya mabingwa Wales na nambari mbili Argentina. Shujaa ilikamilisha makala ya mwaka 2013 katika nafasi ya nne nyuma ya New Zealand, Uingereza na Fiji zilizomaliza katika nafasi tatu za kwanza, mtawalia.

You can share this post!

Wakulima watoa sababu ya wanyakuzi kumezea mate ardhi zao

Kocha mpya wa Simbas atambulishwa

adminleo