• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Anusurika kifo baada ya gari lake kugongana na tingatinga

Anusurika kifo baada ya gari lake kugongana na tingatinga

Na SAMMY WAWERU

MWANAMUME mmoja Jumanne alinusurika kifo gari lake lilipogongana na tingatinga eneo la Progressive, katika barabara inayounganisha mtaa wa Mwihoko na Githurai.

Kwa mujibu wa walioshuhudia tukio hilo, tingatinga lilikuwa limegonga magari mawili zaidi kabla kufikia gari hilo la kibinafsi.

Inasemekana mwendesha tingatinga na aliyeonekana kuzidiwa na makali ya pombe, alikuwa ameonywa na wafanyakazi wenza dhidi ya kuingia barabarani akiwa katika hali aliyokuwa.

“Tumejua hali yake si kamilifu baada ya kugonga gari aina ya Nissan na kujifanya hakuna kilichotokea. Isitoshe, ameendelea na safari, akaangusha tuktuk kabla kufikia kwa hili la kibinafsi,” akaelezea mhudumu wa bodaboda.

Vyuma vya tingatinga na vinavyotumika kuchimba udongo, vililenga upande wa dereva wa gari la kibinafsi, ambapo mlango pia uliharibiwa vibaya.

Licha ya kutakiwa afidie hasara aliyosababisha kwa magari husika, mwendesha tingatinga hakuonekana kujutia chochote. “Ninachosubiri ni askari waje wanikamate,” alieleza kwa ujeri.

Ilichukua juhudi za maafisa wa trafiki wanaohudumu eneo la Githurai, kuingilia kati kisa hicho, na kumtia nguvuni. “Ni hatia kwa dereva yeyote kuendesha gari akiwa mlevi, ninasihi madereva wawe waadilifu,” akashauri afisa wa trafiki aliyejitambua kama Bw Kairu.

Kwa mujibu wa sheria za trafiki, faini ya kuendesha gari ukiwa mlevi haipaswi kuzidi Sh100, 000 au utumikie kifungo cha miaka miwili gerezani, au adhabu zote mbili.

You can share this post!

Mtundu Neymar nje ya kikosi baada ya kujivinjari

BIDIIBUILD: Programu ya kurahisisha ufuatiliaji wa jinsi...

adminleo