• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Magoha na wenzake waitwa bungeni

Magoha na wenzake waitwa bungeni

Na CHARLES WASONGA

WAZIRI wa Elimu Prof George Magoha, Inspekta Jenerali Hillary Mutyambai na Afisa Mkuu Mtendaji wa Tume ya Huduma za Walimu (TSC) Nancy Macharia sasa wametakiwa kufika mbele wa wabunge kuelezea hali iliyochangia kuondolewa kwa walimu Kaskazini Mashariki ya Kenya.

Spika wa Bunge la Kitaifa Justin Muturi Jumanne alisema watatu hao sharti wafike kibinafsi mbele ya Kamati ya Bunge kuhusu Elimu wiki hii na wala wasiwatume wawakilishi wao.

Huku akitaja suala hilo kama la dharura na lenye umuhimu wa kitaifa, Bw Muturi aliitaka kamati hiyo kuwahoji watatu hao ili iwasilishe ripoti bungeni Jumanne juma lijalo.

“Hili ni suala nzito na lenye umuhimu wa kitaifa. Kwa hivyo, linapasa kushughulikia kwa dharura na ripoti iwasilishwe bungeni na kwa Wakenya Jumanne wiki ijayo,” akasema.

Bw Muturi alimwagiza mwenyekiti wa kamati hiyo Julius Melly kuhakikisha kuwa Profesa Magoha na Dkt Macharia wameelezea kamati yake ikiwa uamuzi huo uliidhinishwa na Bodi ya TSC.

“Tunataka kujua ikiwa ni kweli kwamba asasi moja ya serikali ilifanya maamuzi bila kuzingatia sheria ya taratibu. Au ikiwa TSC ilichukua uamuzi huo bila kushauriana na wizara ya Elimu au Idara ya Polisi,” akasema.

Bw Muturi alitoa amri hiyo kufuatia ombi lililowasilishwa na Mbunge wa Wajir Magharibi Ahmed Kolosh aliyetaka maelezo kuhusu sababu iliyopelekea TSC kuwahamisha zaidi ya walimu 1,000 wasio wenye kutoka kaunti za Wajir, Garissa na Mandera.

Bw Kolosh aliyedai kuwasilisha viongozi wa kisiasa kutoaka eneo zima la kaskazini mashariki alilalamika kuhamishwa kwa walimu hao kutaathiri eneo hilo kielimu.

“Tunataka kujua vigezo vilivyotumika kuwahamisha walimu hao na ikiwa Inspekta Jenerali wa Polisi alifahamishwa. Hii kwa sababu hatua hiyo sasa imeathiri masomo katika shule zetu na haswa utekelezaji wa mtaala mpya wa elimu (CBC),” akasema mbunge huyo.

Mwezi Januari, TSC iliwahamisha walimu zaidi ya walimu 1,000 wasio wenyeji wa kaunti za WajiR, Garissa na Mandera kufuatia uvamizi wa kigaidi uliowalenga.

Hii ni baada ya wahalifu waliodaiwa kuwa wafuasi wa kundi la kigaidi la Al Shabaab kuvamia kuwaua walimu watatu katika kituo cha Kamuthe, kaunti ya Garissa.

Hata hivyo, viongozi wa eneo hili wakiongozwa na magavana Ali Korane (Garissa), Ali Roba (Mandera) na kiongozi wa wengi bunge Aden Duale walipinga hatua hiyo wakisema imelemaza masomo katika shule za umma maeneo hayo.

You can share this post!

RIZIKI: Kutoka vibarua vya ujenzi na udobi hadi kumiliki...

EACC lawamani kutompa Sonko ushahidi

adminleo