• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 11:38 AM
Joto lazidi kambi ya Ruto Duale akiandamwa

Joto lazidi kambi ya Ruto Duale akiandamwa

FARHIYA HUSSEIN na VALENTINE OBARA

MWANDANI mwingine wa Naibu Rais William Ruto, Aden Duale, yumo motoni baada ya polisi kuanzisha uchunguzi dhidi yake.

Kiongozi huyo wa wengi katika Bunge la Taifa anachunguzwa kwa madai ya kupeleka chakula kilichooza katika makao ya watoto mjini Garissa.

Hii imeibuka wiki moja baada ya mshirika wake mwingine, Rashid Echesa kukamatwa na kushtakiwa kuhusiana na kashfa ya utoaji wa zabuni feki ya ununuzi wa silaha za kijeshi za thamani ya Sh40 bilioni.

Kwenye uchunguzi huo dhidi ya Bw Duale, kikosi cha maafisa wa polisi, afya, Idara ya Ubora wa Bidhaa (KEBS) na Mamlaka ya Ukusanyaji Ushuru (KRA) walipekua afisi za Hazina ya Kitaifa ya Ustawishaji Maeneobunge (NG-CDF) Garissa Mjini kunakosimamiwa na mbunge huyo.

Imefichuka mbunge huyo, ambaye amekuwa mwandani wa Dkt Ruto kwa muda mrefu, aliagizwa mnamo Jumatano kufika katika ofisi za Idara ya Kuchunguza Uhalifu (DCI) ili aeleze kuhusu malalamishi hayo ambayo ameyakanusha.

“Hakuna ukweli wowote katika suala hilo. Unaweza kwenda Garissa kujionea mwenyewe ukitaka. Nilizungumza na mkuu wa DCI kibinafsi akaniambia hakuna chochote hapo,” Bw Duale aliambia Taifa Leo kwa simu.

Licha yake kukana, Taifa Leo imethibitisha Bw Duale aliambiwa afike mbele ya Benedict Oyaro wa DCI.

Ripoti zilifichua Bw Duale alitembelea makao ya watoto ya Najah, eneo la Bulla Iftin mjini Garissa mnamo Jumatatu wiki hii na akatoa msaada wa vyakula.

“Tulipofungua magunia ya vyakula tuliona vitu vyeusi ndipo tukaingiwa na wasiwasi. Hapo ndipo tuligundua chakula kilikuwa tayari kimeoza,” akasema mmoja wa wahudumu katika kituo hicho.

Ilikuwa mara ya kwanza Bw Duale kutembelea makao hayo ya watoto tangu alipoanza kuwakilisha eneobunge hilo miaka 15 iliyopita.

Meneja wa kituo hicho, Bw Mohammed Noor, alithibitisha kulikuwa na vyakula vilivyopatikana vimeharibika ikiwemo mchele, unga na mahindi.

Imeibuka kuwa chakula hicho kilikuwa kimetolewa na jamii ya Wabohra, ambao walimwomba Bw Duale kuwasaidia kukisambaza kwa wenye mahitaji.

Baada ya kufichuka kwamba chakula kilikuwa kimeoza, maafisa wa jamii hiyo walimtumia ujumbe Bw Duale kuomba radhi wakisema hawakukagua vyakula hivyo kabla kutolewa katika stoo zao.

Kisa hiki kimewafanya wafuasi wa Dkt Ruto kusisitiza kuwa ndio tu wanaolengwa kwa kile wanasema ni kutaka aonekane kuwa mfisadi na pia kuwanyamazisha.

Mwezi uliopita walilalamika wakati Bw Mwangi Kiunjuri aliposimamishwa kazi ya Waziri wa Kilimo, na baada ya Bw Ferdinand Waititu kuvuliwa cheo chake cha ugavana Kiambu.

Jumapili, Bw Kiunjuri aliyendamana na viongozi wengine wa kikundi cha Tangatanga akiwemo Mbunge wa Gatundu Kusini Moses Kuria katika ibada Nanyuki, alimkashifu Rais Uhuru Kenyatta akidai anadhulumu wakosoaji wake.

“Leo hii Kiunjuri na Kuria wakisimama waseme barabara za Laikipia ni mbovu na zinapasa kutengenezwa, kesho yake watakujiwa na DCI, KRA na EACC,” akasema Bw Kiunjuri.

Bw Kuria pia anaandamwa na kashfa kadhaa ikiwemo madai ya kufuja pesa za Hazina ya Ustawi wa Maeneobunge (NG-CDF).

Viongozi wengine ambao wandani wa Naibu Rais wanaamini waliadhibiwa na serikali kuu ni pamoja na aliyekuwa Waziri wa Fedha Henry Rotich, ambaye alishtakiwa kwa uporaji wa fedha za miradi ya mabwawa ya Arror na Kimwarer mwaka jana.

Naye Mbunge Kimani Ngunjiri (Bahati) alipokonywa silaha huku walinzi wa mwenzake Alice Wahome (Kandara) wakiondolewa, naye na Ndindi Nyoro (Kiharu) akakamatwa mwaka jana kwa madai ya kuzua rabsha kanisani.

You can share this post!

Mganga azirai mkewe alipookoka

Raha mitandaoni mwanamume kutoweka na hongo ya polisi Embu

adminleo