• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Familia yalilia haki ya mtoto wao aliyegongwa na gari

Familia yalilia haki ya mtoto wao aliyegongwa na gari

Na SAMMY WAWERU

JUMAPILI Machi 8, 2020, mtoto Njeri alirauka alfajiri na mapema ili kujiandaa kuhudhuria ibada ya kanisa, misa ya watoto katika kanisa la PEFA Progressive eneobunge la Ruiru.

Asubuhi hiyo, mamake anasema alitangamana na watoto wenzake kwenye ploti na kama ilivyo kawaida wakacheza kabla kuelekea kanisani.

Walipoagana, mamake mtoto huyo wa darasa la pili, gredi ya pili chini ya mfumo wa kisasa wa elimu, uamilifu, ndio CBC, alikuwa katika harakati za kufua nguo.

Mwendo wa sita hivi za mchana, alipigiwa simu akiarifiwa kuwa mwanawe amehusika katika ajali na kwamba amepelekwa katika Hospitali ya St John iliyoko Githurai.

“Tulipofika pamoja na babake tulipata mwili ukiingizwa katika gari la polisi ili kupelekwa mochari,” mama huyo aliyezidiwa na huzuni akaambia Taifa Leo.

Alisema alifariki wakati akipelekwa hospitalini.

Inasemekana siku ya tukio, Njeri, 8, pamoja na watoto wenza walikuwa wakitoka kanisani.

“Walivuka barabara kwa kundi, na ndiye alikuwa wa nyuma, wakati gari lililoonekana kuendeshwa kasi lilipompiga dafrau,” akaeleza mmoja wa wakazi aliyeshuhudia.

Gari la kibinafsi lililosababisha maafa ya mtoto huyo lenye nambari ya usajili KCW 923X lilikuwa likiendeshwa na mama.

Inasemekana alikuwa akipeleka mwanawe hospitalini.

Kati ya eneo la ajali, kuna matuta mawili, pembezoni likiwa ni kanisa la PEFA na ambalo kila Jumapili hufurika washirika. Isitoshe, mita kama hamsini hivi kuelekea Githurai barabara hiyo imejipinda.

“Kandokando mwa barabara kuna ploti za kupangisha, magari hayaendeshwi kwa kasi na lazima dereva awe makini kwa kuwa ni eneo lenye idadi kubwa ya watu,” akasema mhudumu mmoja wa tuktuk.

Gari lililosababisha maafa ya mtoto Njeri lilipelekwa katika kituo cha polisi cha Kahawa Wendani, ambacho kina kitengo cha trafiki na kufikia sasa familia ya marehemu inalilia haki ikidai hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa.

Inasemekana mama aliyesababisha kifo cha mtoto wao aliachiliwa huru, ingawa gari limezuiliwa kituoni.

Afisa mmoja wa polisi na aliyeomba tusichapishe jina lake kwa sababu haruhusiwi kuzungumza na waandishi wa habari, alisema hatua ya kwanza ni gari kuzuiliwa kituoni ili kufanyiwa uchunguzi kubaini ikiwa inaruhusiwa kuwa barabarani.

“Uchunguzi umeanzishwa kujua iwapo imeafiki sheria za trafiki, ikiwamo kuwa na bima na ukaguzi wa kina (inspection),” akasema.

Pia alisema dereva atachunguzwa ikiwa amehitimu mafunzo ya udereva na kuwa na leseni ili kufunguliwa mashtaka.

You can share this post!

KRU yasimamisha msimu 2019-2020 kwa sababu ya COVID-19

Corona yayumbisha utalii baada ya safari kusitishwa

adminleo