• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
AKILIMALI: Ndizi ni uwekezaji wa maana, panda kwa wingi

AKILIMALI: Ndizi ni uwekezaji wa maana, panda kwa wingi

Na JOHN NJOROGE

[email protected]

Kwa safari ya kilomita 10 kutoka kituo cha magari cha Cheponde katika barabara ya Molo- Nakuru, tunapitia kwa njia nyembamba ambayo ni mbovu, inayopitia katikati ya shamba la Cheponde mjini Elburgon na kutufikisha nyumbani kwake Timothy Gachie na kumpata akiwa kazini katika shamba lake lililoko Keriko eneo la Rongai katika kaunti ya Nakuru.

Huku amevalia shati ya kahawia, suruali ya kijivu na viatu vya kazi, Gachie alikuwa akiangalia na kuzunguka kwa miti ya ndizi yake iliyoharibika.

Kando kidogo, wake wawili wa mzee Gachie walikuwa wanakata nyasi na matawi ya viazi vitamu kwa ng’ombe wao wa maziwa.

Gachie ni dereva mstaafu wa malori ambaye kwa sasa hujihusisha na ukulima wa kikuu kwa shamba lake la ekari nane ambazo amezigawanya kwa sehemu tofauti. Kati ya hizo ekari nane, nusu ekari ameitenga kwa upanzi wa ndizi ambayo anakuza kwa wingi.

“Nilipokuwa nafanya kazi katika nchi ya Uganda, nilitambua kuwa mwajiri wangu alikuwa na shamba kubwa ambalo alipanda ndizi nyingi. Akiwa shambani la mwajiri wake, aligundua kuwa hakuwa na kazi nyingi aliyoifanyia kwa shamba lake la ndizi,’’ akasema Gachie.

Alisema bosi wake alihakikisha ndizi zake hupata maji ya kutosha na pia kukata matawi ya shina yaliyokua kupita kiasi.

Wakati Gachie alistaafu miaka sita iliyopita, alianza ukulima wa ndizi na kwa vile shamba lake ni kubwa, alitenga sehemu na kupanda miti ama shina ya ndizi aliyoitoa nchi ya Uganda.

“Ukulima wa ndizi ndio rahisi kwa mkulima yeyote. Maji na mbolea pekee ndiyo huhitajika katika msimu wa kupanda,’’ akasema Gachie.

Kwa muda wa mwaka mmoja, mkulima huyu alisema miti ya ndizi huanza kuibuka na rangi ya zambarau huanza kuonekana katika sehemu ambayo ndizi huchipukia.

Hata hivyo, Gachie alisema maji na mbolea nyingi husabambisha miti ya ndizi kumea na kukua kwa upesi.

“Kwa wakati huu, mkulima hustahili kutoa matawi ama sehemu za miti ya ndizi (suckers) zilizokua kupita kiasi,’’ akasema na kuongeza kuwa aliendelea kunyunyizia mbolea kwa miti ya ndizi ilipokuwa ikikua.

Wakati wa matayarisho ya shamba, wakulima wa ndizi huagizwa kulima shamba wakati wa kiangazi ili kutokomeza magugu na kupata wasaa mzuri wa kupanda wakati mvua ndefu inapoanza.

Kulingana na idara ya kilimo, ukubwa wa mashimo unapopanda wakati wa kiangazi hufaa kuwa 90 kwa 90 kwa 90 cm na 60 kwa 60 kwa 60 cm katika sehemu zilizoko na mvua.

Afisa mmoja ambaye ni mtaalamu wa wadudu na magonjwa na ambaye aliomba tulibane jina lake alisema kuwa wadudu kama vile Banana Weevil, Nematodes na Banana Silvering Thrips ndio huvamia ndizi mara nyingi.

“Wadudu kama vile Banana Weevils hutegwa kwa kutumia vipande vya shina vilivyozeeka nazo Banana Silver Thrips hunyunyiziwa dawa ya wadudu,’’ akasema.

Alisema kuwa magonjwa yanayo athiri ndizi ni kama vile Cigar, End Rot, Panama, Sigatoka Leaf Spot, Bacterial Xanthomas Wilt, Black leaf Streak, Bunchy Top na Anthracnose baadhi ya magonjwa mengine.

Gachie amepanda migomba mia nne (400) katika shamba lake lakini mia mbili (200) kati ya hayo yaliharibika wakati mvua ya mafuriko ilinyesha hivi majuzi.

“Nilipata hasara zaidi ya laki mbili wakati wa mafuriko hayo ambapo nilitarajia kupata zaidi ya milioni mbili baada ya mauzo katika mwisho wa mwaka huu,’’ akasema huku akionyesha baadhi ya ndizi zilizoharibiwa.

Gachie alifichua kuwa yeye huuza ndizi zake ndani ya nchi kwa wafanyabiashara wadogo wadogo kwa shilingi elfu moja na kumlipa mfanyi kazi wake anayewatunza na kuyafanya kazi kwa shilingi mia mbili kwa siku.

Kulingana naye ndizi hazina msimu wa kuvuna hasaa zikiwa zimepata mbolea ya kutosha.

Mkulima huyu anakumbuka siku moja ambapo alipata elfu hamsini (50,000) kwa mauzo ya ndizi ambazo alisema kuwa ndio kiwango cha juu sana kwa mkulima wa ndizi kupata kwa siku moja.

“Serikali kuu na zile za kaunti hufaa kutengeneza na kutafuta soko kwa wakulima wa ndizi ilikuuza mazao yao kwa bei nafuu,’’ akasema.

Gachie amechiba bwawa ndogo ambapo yeye hutumia magomba anaponyunyizia maji.

Gachie amewekeza pakubwa kwa ukulima wake wa ndizi ambapo aliongeza kuwa aliacha ukulima wa mahidi ili kujishughulisha na ukulima wa ndizi.

“Mahindi yana kazi nyingi kabla ya muda wa kuvuna kufika. Afadhali nipande vyakula vya miezi michache kuliko nipande mahidi,’’ akasema.

Alikiri kuwa hata ingawa ana shamba kubwa ambalo angelitumia kufuga mifugo, aliacha ufugaji wa ng’ombe za maziwa na kuingia kwa kilimo.

Gachie pia hupanda vitunguu, mboga, pilipili, dania baadhi ya zingine.

Wakulima wengi katika maeneo ya Elburgon na Molo wameacha kilimo cha mahidi ambacho huchukua muda mrefu kabla mavuno na kujiingiza na kilimo biashara.

Katika ukulima huu, mkulima hupanda vyakula vyake katika sehemu ndogo ambayo humpa mapato mazuri.

You can share this post!

AKILIMALI: Waanzisha kiwanda cha bishara ya nyama ya sungura

Wahudumu wa bodaboda wa kijiji cha Githogoro wamlilia Mungu

adminleo