• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
Manvir Baryan ashinda mbio za magari Afrika Kusini

Manvir Baryan ashinda mbio za magari Afrika Kusini

Na GEOFFREY ANENE

MKENYA Manvir Baryan ameibuka mshindi wa mbio za magari za Afrika duru ya Afrika Kusini, Jumamosi.

Baryan, ambaye alitawazwa mfalme wa Mbio za Magari za Afrika mwaka 2017 akishirikiana na mwelekezi wake Drew Sturrock katika gari la aina ya Skoda Fabia, alianza duru hii ya tatu kwa kumaliza sehemu ya kwanza katika nafasi ya sita.

Hata hivyo, aliimarika na kushinda sehemu za pili na tatu, akatupwa nafasi ya nane katika sehemu ya nne, akarejea nambari moja sehemu ya tano, akateremka hadi nambari tatu sehemu ya sita na kumaliza mkondo huo wa kwanza uliojumuisha kilomita 105.9 kwa kushikilia nafasi ya sita katika sehemu ya saba.

Alianza mkondo wa pili na lala salama kwa kurukia nambari mbili katika sehemu ya nane na kuteremka nafasi moja katika sehemu wa tisa. Alitawala sehemu ya 10 na kumaliza sehemu ya 11 katika nafasi ya tatu. Alishinda sehemu ya 12 na tena 13 na 14 na 15 (mwisho). Mkondo wa pili ulijumuisha kilomita 114.6.

Baryan alikamilisha mbio hizi za kilomita 220.5 kwa saa 2:47:43.9, dakika 3:14 mbele ya mabingwa wa duru hii ya Afrika Kusini mwaka 2017 Guy Botterill aliyeshiriikiana na Simon Vacy-Lyle katika gari la aina ya Toyota Etios.

Mathew Vacy-Lyle na mwekelezi wake Rikus Fourie waliridhika katika nafasi ya tatu pia wakiendesha Toyota Etios.

Walifuatwa na Leroy Gomes/Riyaz Latife (Mitsubishi Evo 9), AC Potgieter/Nico Swartz (Volkswagen Polo), JJ Potgieter/ Tommy du Toit (Ford Fiesta), Kleevan Gomes/Zunaid Khan (Mitsubishi Evo 9), Lee Rose/Elvene Vonk (Ford Escort), Tjaart Conradie/Mari van der Walt (Toyota Elios) nao Jacques du Toit na mwelekezi wake Ronald Rens wakafunga 10-bora (Volkswagen Polo).

Madereva 30 walianza mashindano, lakini 17 pekee ndiyo walimaliza. Wengine walijiuzulu katika sehemu mbalimbali za mashindano kutokana na matatizo mbalimbali.

Ushindi wa Manvir unafufua matumaini yake ya kutetea taji lake hasa baada ya kukosa kumaliza duru ya Afrika ya Safari Rally mwezi Machi nchini Kenya injini ya gari lake ilipojaa maji.

You can share this post!

Jopo maalum kuundwa kufanikisha muafaka wa Uhuru na Raila

Matokeo duni yazidi kumwandama Okumbi

adminleo