• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 10:55 AM
KAFYU: Mji wa Thika wageuka mahame

KAFYU: Mji wa Thika wageuka mahame

Na LAWRENCE ONGARO

WAKAZI wa Thika walitii agizo la serikali kwa kurejea nyumbani mapema ili wasije wakakwaruzana vibaya na maafisa wa usalama.

Ilipofika saa tisa alasiri mnamo Ijumaa wafanyabiashara wengi walianza kufunga maduka yao huku wakijiandaa kuabiri matatu mapema ili kurejea nyumbani.

Ilipofika saa kumi na mbili na nusu za jioni mji wa Thika ulionekana mahame huku kila mwananchi akiwa amerejea nyumbani kuepukana na walinda usalama.

Naibu kamishna wa Thika Magharibi Bw Douglas Mutai amesema ameridhika na jinsi ambavyo wakazi wa Thika walitii serikali bila kulazimishwa.

“Maafisa wa usalama walipiga doria usiku wote hadi alfajiri ambapo barabara zote zilikuwa mahame huku kila dula la kibiashara likiwa limefungwa kabisa. Iwapo wananchi watafuata maagizo yote ya serikali bila shaka tutaweza kudhibiti Covid-19,” amesema Bw Mutai.

Amesema baadhi ya masoko makubwa katika Kaunti ya Kiambu yamefungwa ili kukabiliana maambukizi ya virusi vya corona.

Baadhi ya masoko yaliyofungwa wiki hii ni Madaraka, Makongeni, Jamhuri, Ruiru, na Githurai.

“Lengo letu kuu ni kuona ya kwamba wananchi wanafuata maagizo yote wanayopewa na serikali ili kuangamiza janga hili la Corona,” amesema Bw Mutai.

Amepogeza juhudi ambazo zimechukuliwa na wahisani kadha mjini Thika kwa kutoa mitungi ya kuhifadhi maji, dawa, na sabuni ya kutumika wakati wa kunawa mikono.

Amesema tayari amewafahamisha machifu wafanye juhudi kuona ya kwamba wanawahamasisha wananchi kila mara mashinani ili wanawe mikono.

Amesema kwa muda wa wiki mbili sasa mji wa Thika umegeuka mahame kwa sababu biashara chache ndizo zinaendelea huku ofisi nyingi za serikali zikiwa zimefungwa.

Biashara chache

Leo Jumamosi biashara chache mno ziliendelea mjini Thika kwani maduka mengi yamesalia kufungwa huku wafanyabiashara wengi wakiamua kubaki nyumbani.

Uchunguzi uliofanywa unaonyesha ya kwamba mikahawa mikubwa, na maduka kadhaa hayakufunguliwa kwani kafyu ya Ijumaa iliwapa watu wengi hofu huku wengine wakisafiri kutoka mbali ili kufungua biashara zao.

Baada ya kushuhudia yale yaliteyondeka Ijumaa usiku wengi wa wafanyabiashara wamesisitiza wataendelea kufunga maduka yao kuanzia mwendo wa saa kumi za jioni ili kupata muda wa kutosha kufika nyumbani na kujumuika na familia zao.

“Mimi leo nitafanya juhudi kuona ya kwamba ninarejea nyumbani mapema ili nitulie kwangu taratibu bila mabishano na yeyote,” amesema James Mungai ambaye ni muuzaji wa simu katika duka moja mjini Thika.

Hata matatu nyingi hazikuonekana mjini Thika kwani wamiliki wengi wameamua kwanza watulie wajionee mambo yalivyo kwani wanasema bado wanapata hasara kwa sababu ya kubeba abiria wachache.

You can share this post!

AKILIMALI: Kinyozi mwanadada ambaye wateja wake wa mwanzo...

UKUMBI WA LUGHA NA FASIHI: Alama za uakifishaji ambazo kila...

adminleo