• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Binti apiga hatua katika biashara ya bima licha ya changamoto

Binti apiga hatua katika biashara ya bima licha ya changamoto

PAULINE ONGAJI

Sio wengi wanaweza kumudu huduma za bima hapa nchini. Na hii ni mojawapo ya sababu zilizomsukuma Bi Wanjiru Githiomi, 45, kuanzisha kampuni ya BimaNet, jukwaa linaloshirikiana na kampuni za bima ili kutoa huduma hii kwa bei nafuu.

Ni huduma ambayo hasa inalenga watu binafsi na biashara ndogo ambapo wamekuwa wakishirikiana na zaidi ya wasambazaji 60 wa huduma za bima wanaotangaza bidhaa hii hasa kwa biashara ndogo.

“Naweza sema kwamba huduma hii inawapa watu binafsi, na wamilikia wa biashara ndogo, kupokea huduma hii,” aeleza.

Kulingana naye, BimaNet pia imeshirikiana na mashirika kadhaa ya bima na kulingana na mapato yao, wanachangia katika hazina ya kusaidia kuelimisha wanafunzi kutoka familia maskini.

“Pia, tuko katika harakati za kushirikiana na majukwaa mengine kama vile makanisa, taasisi za kimasomo, vyama, sacco miongoni mwa mengine iliyo na wanachama wanaokaribiana na vikundi tunavyolenga,” asema.

Mpangilio wao wa kipekee wa kibiashara unawawezesha kupunguza gharama ya kutoa huduma hii na hivyo kupitisha kipunguzio hiki kwa wateja na washirika wao. “Aidha, mawakala wa bima na mabroka wetu wanapata vipunguzio vya juu kumaanisha kwamba kila mtu ananufaika,” aongeza.

Kulingana naye, changamoto kuu imekuwa kupata wauzaji. “Aidha, Wakenya kwa ujumla hawatambui umuhimu wa bima ya maisha kwa sababu wengi wetu hutegemea harambee ili kuchanga pesa, kila tunapokumbwa na majanga,” aeleza.

Pia, mkurupuko wa maradhi ya COVID-19 umesababisha hasara kubwa katika biashara hii. “Lakini badala ya kufa moyo na kuishiwa nguvu, tumeamua kutumia wakati huu kuunda mikakati ya kutumia fursa hii kujiimarisha. Pindi baada ya mawimbi haya kupita, tunaamini kwamba bima ya afya itakuwa mojawapo ya bidhaa zitakazohitajika sana na wengi,” aeleza.

Pia anazungumzia changamoto ya kusawazisha muda wa kukaa nyumbani kwake jijini Cape Town, na pia kuendesha biashara nchini Kenya.

Bi Githiomi ambaye ni mkazi wa Afrika Kusini, alizaliwa na kusomea humu nchini kabla ya kujiunga na Chuo Kikuu cha Cape Town, nchini Afrika Kusini ambapo alisomea masuala ya sheria.

Baadaye alihudumu katika Nyanja ya sheria kwa mwaka mmoja unusu kabla ya kujitosa katika taaluma ya mauzo na udhamini na kuanzisha kampuni yake kwa jina Leverage Inc. Hata hivyo, aliuza biashara hii miaka mitatu iliyopita, alipohitaji mtaji wa kuanzisha biashara yake mpya nchini Kenya.

Anasema kwamba kamwe hajutii kuacha kazi iliyokuwa na mapato na kujitosa katika ujasiriamali. “Uamuzi huo ulinisaidia kujivunia kipato kizuri, huku ikiniachi muda wa kuwa mama na mke,” aeleza.

You can share this post!

Lamu yashangaza kutumia maji ya bahari kukabili corona

Sakaja kuongoza kamati ya seneti kuhusu janga la corona

adminleo