• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 9:40 PM
Msipore fedha za corona – Weta

Msipore fedha za corona – Weta

Na DENNIS LUBANGA

KIONGOZI wa Chama cha Ford Kenya Moses Wetang’ula, amesema kwamba fedha zilizotengwa kusaidia kupigana na janga la corona zinafaa kutumika kwa uwazi badala ya kuporwa na watu wachache wenye tamaa serikalini.

Seneta huyo wa Bungoma alisema serikali kuu na zile za kaunti zinafaa kutumia fedha hizo vizuri ili kusitokee hali kama siku za nyuma ambapo ufichuzi wa sakata mbalimbali za ufujaji wa fedha zilitokea baada ya majanga nchini.

“Matumizi mabaya ya fedha za kupigana na janga la corona ni kosa la kihalifu,” akaeleza Taifa Leo jana.

Alitoa wito kwa afisi ya Mkaguzi wa hesabu za serikali, kamati za uhasibu bungeni na kwenye magatuzi mbalimbali pamoja na vitengo vya serikali kufuatilia kwa makini jinsi fedha hizo zinavyotumika.

“Hapa nchini wizi wa pesa za umma hukithiri sana wakati wa majanga kama haya. Mtindo huu wa mambo unafaa ukomeshwe kwa sababu pesa hizo zinafaa kusaidia Wakenya,” akaongeza Bw Wetang’ula.

Aidha alisema kwamba ziara yake kwenye baadhi ya hospitali za kaunti ilimdhihirishia kwamba hakuna vifaa vya kutosha za kuwahudumia wagonjwa.

“Lazima fedha zilizotolewa na Benki ya Dunia kwa serikali kuu pia zigawiwe kaunti ili kuimarisha sekta yao ya kiafya. Hii kaunti ina hospitali chache sana ambazo zina vifaa vya kutosha na iwapo hali itazidi kuwa mbaya basi tutakuwa taabani,” akasema.

Kauli ya seneta Wetang’ula linajiri wakati ambapo serikali inaendelea kupokea fedha kutoka masharika mbalimbali ndani na nje ya nchi ili kuisadia kupigana na janga la corona

Vilevile Bw Wetang’ula aliirai Wizara ya Afya kuanza kuwapima Wakenya katika maeneo mbalimbali ili kuzuia virusi hivyo visienee zaidi.

You can share this post!

WHO yaonya huenda Afrika ikawa kitovu cha maambukizi ya...

Msifanye mzaha na corona – Raila

adminleo