• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 10:55 AM
UHABA: Foleni ndefu wachukuzi wenye mikokoteni wakitafuta maji mtaani Kariobangi South Civil Servants

UHABA: Foleni ndefu wachukuzi wenye mikokoteni wakitafuta maji mtaani Kariobangi South Civil Servants

Na GEOFFREY ANENE

SI kawaida kuona mamia ya mahamali kufika mtaani Kariobangi South Civil Servants kwa siku moja.

Hata hivyo, mambo yalikuwa tofauti Mei 10 pale wafanyabiashara hao wa kuchota maji na kuyauza walipomiminika katika kisima kimoja mtaani hapa kutokana na uhaba wa maji unaotatiza jiji la Nairobi.

Wengi waliofika hapa walitoka mtaa huu pamoja na mitaa jirani ya Mutarakwa, Kariobangi South, Dayspring, Doctor Mwenje, Gaza na Baraka na pia sehemu kadhaa za Umoja III.

Mitungi ya maji inaoshwa sokoni kabla ya kuuziwa wateja wakiwemo wachukuzi wenye mikokoteni. Picha/ Geoffrey Anene

Kutoka saa mbili asubuhi Jumapili hadi saa kumi na mbili na nusu jioni, shughuli ya kuhudumia wenye mikokoteni ilikuwa ni kibarua cha ziada kwa Bwana Ndegwa, ambaye ni mmiliki wa kisima hicho alichochimba Mei 2015.

Wateja hao walifika hapa na mitungi ya lita 20.

Wao huuziwa mtungi mmoja katika kisima hiki kwa Sh5.

Mmoja baada ya mwingine, waliwasili hapa, kila mmoja na mkokoteni uliojaa kati ya mitungi 20 na 30, ambayo wanauzia wateja kwa kati ya Sh30 na 40 kila mtungi.

Mkokotaji wa mkokoteni asafirisha mitungi ya maji ya lita 20 kuoshwa kabla ya kutumiwa na wachukuzi kuchota na kuuzia wateja katika mitaa ya Nairobi. Picha/ Geoffrey Anene

Mhudumu mmoja wa kisima hicho alieleza Taifa Leo kuwa kwa siku ya kawaida wao huuza kati ya lita 70,000 na 90,000 za maji kila siku.

“Leo ilikuwa siku tofauti kabisa kwa sababu tuliuza zaidi ya mara tatu ya lita tunazouza kila siku. Kuna visima kadhaa mbali na hiki hapa ambavyo wenyewe hawakufungua biashara. Pia, kuna uhaba wa maji jijini Nairobi. Kutoka Alhamisi, wakazi wamekuwa wakitatizika masuala ya maji, ingawa umati huu nimeushuhudia tu leo. Kutoka asubuhi sijapumzika kwa sababu ya foleni hii ndefu unaona hapa,” alisema mhudumu huyo, ambaye alifichua kuwa aliraushwa saa kumi na mbili asubuhi na mteja wa kwanza kabla ya foleni ya wenye mikokoteni kuanza kushuhudiwa dakika chache tu baada ya saa mbili asubuhi.

You can share this post!

Obama akosoa hatua za serikali ya Trump kukabili Covid-19

MALIPO DUNI: Wanasoka wanawake timu ya taifa ya Amerika...

adminleo