• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 12:58 PM
Kampuni ya Wachina ya Sinohydro yawapa chakula wakazi wa Thika Mashariki

Kampuni ya Wachina ya Sinohydro yawapa chakula wakazi wa Thika Mashariki

Na LAWRENCE ONGARO

KUNA haja ya kuwajali watu wanaohitaji chakula hasa wakati huu taifa na ulimwengu mzima unaposhuhudia janga la Covid-19.

Naibu kamishna wa Thika Mashariki, Bw Thomas Sankei, ametoa wito kwa mashirika yaliyo na uwezo yawajali watu walioathirika na ambao hawana chakula.

Alisema hayo wakati akiipongeza kampuni ya Sinohydro Corporation ambayo ilijitokeza wazi na kuwapa chakula wakazi zaidi ya 300 katika eneo la Kilimambogo ambako kumetundikwa kizuizi kinachowazuia wasafiri kuelekea kaunti za Machakos na Murang’a.

Kamishna wa Thika Mashariki Thomas Sankei akisambaza barakoa kwa wakazi wa eneo la Ngoliba. Picha/ Lawrence Ongaro

Mnamo Jumamosi kampuni hiyo ya Wachina ya kusaga kokoto na mawe, ilitoa chakula ambapo wakazi hao walipokea unga wa ugali, mafuta ya kupikia na hata sabuni ya kuogea.

“Naishukuru sana kampuni hiyo kwa kazi nzuri wameonyesha ya kuwajali wakazi wa Kilimambogo eneo la Ngoliba kwa kuwapa chakula,” alisema Bw Sankei.

Kizuizi kilichowekwa, walisema, kimewazuia wakazi wengi kutembea kwenda maeneo mengine kwa shughuli za kujitafutia chakula.

Baadhi walisema kinachowapa afueni kidogo ni kwamba walibakisha chakula kidogo walichovuna msimu uliopita.

Wakazi hao wametoa mwito kwa wahisani popote walipo wafanye juhudi ili kuwapa chakula haraka iwezekanavyo.

Wakazi wengi katika eneo hilo wanafanya kazi za mashamba na katika kampuni ya uchimbaji mawe iliyoko hapo karibu.

Bw Sankei alisema wakazi hao wanaishi katika maisha ya kipato cha chini na kwa hivyo wanahitaji misaada kwa wingi.

“Mimi kama afisa wa serikali eneo hili natoa mwito kwa wahisani hasa wafanyabiashara wengi walio Thika Magharibi, wajitokeze na kusaidia watu wangu wa upande huu wa Mashariki ambako mara nyingi huwa kukavu,” akasema afisa huyo.

You can share this post!

Klabu za La Liga zataka soka ya Uhispania irejelewe Juni 8...

Sofapaka wataka AFC Leopards waombe msamaha kwa kuwadunisha

adminleo