• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 12:26 PM
Strathmore Leos kusajili wachezaji watano

Strathmore Leos kusajili wachezaji watano

Na CHRIS ADUNGO

VIONGOZI wa jedwali la Ligi ya Daraja la Kwanza la Raga ya Kenya (Championship), Strathmore Leos wamefichua azma ya kusajili wachezaji watano kadri wanavyopania kujisuka upya kwa minajili ya kampeni za msimu ujao.

Haya ni kwa mujibu wa kocha Louis Kisia ambaye amekariri kwamba tayari wametambua wanaraga hao wanaopania kujinasia huduma zao kutoka vikosi ambavyo ni wapinzani wao katika kivumbi cha Championship.

“Tunalenga kuimarisha zaidi idara yetu ya ushambuliaji ambayo imekuwa ikitukosesha usingizi kwa kipindi kirefu. Azma yetu ni kuwapiga jeki mafowadi waliopo ili kuweka hai matumaini ya kufuzu kwa Ligi Kuu ya Kenya na kutia fora katika kipute hicho,” akasema Kisia.

Hadi raga ya humu nchini iliposimamishwa mnamo Machi 2020 kutokana na janga la corona, Leos walikuwa wamejizolea jumla ya alama 76 kutokana na jumla ya 80 ambazo walikuwa na uwezo wa kutia kapuni.

“Nimeridhishwa na jinsi ambavyo tumecheza hadi kufikia sasa msimu huu. Kiu ya kusajili ushindi katika kila mechi na ari ya kutawala kila mchuano ni zao la msukumo wa kutaka kurejea katika Ligi Kuu baada ya kuteremshwa ngazi muhula jana,” akaongeza Kisia ambaye ni mwanaraga wa zamani wa Mwamba RFC.

Chini ya ukufunzi wake, Leos hawajazidiwa maarifa katika mchuano wowote kati ya 16 iliyopita.

Hadi kusitishwa kwa raga ya humu nchini, Leos walikuwa wameratibiwa kuchuana na mshindi kati ya Northern Suburbs na wasomi wa USIU-A kwenye nusu-fainali ya Championship.

Kwingineko, Mwamba RFC wamefichua kwamba Samurai Sportswear ndio watakaokuwa wadhamini wa jezi zao katika msimu huu wa 2020-21. Wanaraga wa Mwamba kwa sasa wataacha kuvalia jezi za BLK zilizotumiwa na kikosi hicho kwa minajili ya msimu wa 2019-20.

You can share this post!

Ayimba sasa ni mkurugenzi wa kiufundi RLF

Wachezaji wa Gor hawajalipa kodi kwa miezi 5 – Rachier

adminleo