• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 4:55 PM
Gathimba kuwania mamilioni Matembezi ya Dunia Uchina

Gathimba kuwania mamilioni Matembezi ya Dunia Uchina

Na GEOFFREY ANENE

SHIRIKISHO la Riadha Duniani (IAAF) limetangaza zawadi nono kwa wanariadha watakaoshindana kwenye Matembezi ya Dunia ya Kilomita 20 mjini Taicang, Uchina, Mei 5-6, 2018.

Kenya inawakilishwa na mshindi wa medali ya shaba ya Michezo ya Jumuiya ya Madola, Samuel Gathimba.

Tuzo za binafsi ni Sh3,013,725 kwa mwanamedali wa dhahabu, Sh1,506,862 (fedha) na Sh1,004,575 (shaba). Nambari nne hadi sita watatia mfukoni Sh703,202, Sh502,287 na Sh301,372, mtawalia.

Tuzo za timu ni Sh1,506,862 (mabingwa) nao nambari mbili hadi sita watatunikiwa Sh1,205,490, Sh904,117, Sh753,431, Sh602,745 na Sh301,372. Mtembeaji atakayevunja rekodi ya duniani, atapata bonasi ya Sh502,2875.

Mjapani Yusuke Suzuki anashikilia rekodi ya dunia ya wanaume ya saa 1:16:36 aliyoweka katika Riadha za Bara Asia mwaka 2015 nchini Japan. Mshikilizi wa rekodi ya dunia ya matembezi ya kilomita 20 kwa wanawake ni Mchina Liu Hong. Anajivunia kukamilisha umbali huo kwa saa 1:24:38 mwaka 2015 nchini Uhispania.

Watembeaji 386 kutoka mataifa 49 watashiriki makala ya mwaka 2018.

Ni mara ya kwanza Kenya inashiriki matembezi haya tangu Patrick Mokomba, Mutisya Kilonzo, William Sawe na Isaac Kiplimo wamalize makala ya mwaka 1989 katika nafasi za 74, 78, 96 na 98 mtawalia kutoka orodha ya washiriki 130 mjini Catalunya nchini Uhispania.

Gathimba, 41, alishindia Kenya medali ya matembezi ya Jumuiya ya Madola alipokamilisha nyuma ya Dane Bird-Smith (Australia) na Muingereza Tom Bosworth kwa saa 1:19:51 mjini Gold Coast mnamo Aprili 8.

Muda wake ulikuwa sekunde 49 nje ya rekodi ya Afrika inayoshikiliwa na Mtunisia Hatem Ghoula tangu mwaka 1997.

You can share this post!

Kibarua kwa Obiri mita 3,000 Diamond League

Raila atangaza mwisho wa ‘Resist’

adminleo