• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Mmoja afariki katika ajali Limuru

Mmoja afariki katika ajali Limuru

Na MARY WANGARI

MTU mmoja amefariki Jumatano abiria wengine kadhaa wakiuguza majeraha mabaya kufuatia ajali iliyohusisha matatu na lori la mchanga katika eneo la Mutarakwa, Limuru, Kaunti ya Kiambu, mnamo Jumatano.

Ajali hiyo ilitokea mwendo wa saa tatu asubuhi dereva wa matatu hiyo iliyokuwa ikielekea eneo la Ndeiya kutoka Limuru aliposhindwa kuidhibiti, kulingana na Kamanda wa Polisi katika Kituo cha Polisi cha Tigoni, Bw Joseph Ireri aliyezungumza na Taifa Leo.

Afisa huyo ameeleza kuwa matatu hiyo ilipoteza mwendo na kugongana na lori la kusafirishia mchanga kwenye barabara kati ya Mai Mahiu – Nairobi.

Aidha, alieleza kuwa majeruhi katika ajali hiyo walipelekwa katika Hospitali ya Limuru Nursing Home almaarufu ‘Kwa Patel.

“Dereva alishindwa kudhibiti gari hilo; tumepoteza mtu mmoja na majeruhi wamepelekwa katika kituo cha afya cha Limuru Nursing Home kwa matibabu,” amesema Bw Ireri.

Afisa huyo aliwahimiza madereva kuwa waangalifu na kuhakikisha magari yao hayana hitilafu yoyote wanaposafirisha abiria, akiongeza kuwa uchunguzi umeanzishwa kubaini kiini cha ajali hiyo.

Kisa hicho kimejiri huku ajali katika barabara hiyo inayounganisha eneo la Mutarakwa na Thogoto, Kikuyu, zikizidi kuongezeka kwa kasi eneo hilo na kuibua wasiwasi miongoni mwa wakazi.

Waendeshaji magari wameelekezewa kidole cha lawama kwa kukosa uangalifu kwenye barabara hiyo yenye shughuli nyingi.

You can share this post!

Changamoto kutokana na janga la corona zayumbisha wachezaji...

Obiri, Kipruto wapata vibali vya kunogesha kivumbi cha...

adminleo