• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 4:55 PM
AFYA: Barakoa chafu zinavyosambaza corona vijijini

AFYA: Barakoa chafu zinavyosambaza corona vijijini

Na LEONARD ONYANGO

VIDEO ya mwanaume aliyeonekana akisafisha barakoa zilizotumika iliwatia hofu Wakenya ilipochipuza katika mitandao ya kijamii miezi mitatu iliyopita.

Katika video hiyo, mwanaume huyo alionekana akisafisha rundo la barakoa zilizotumika kwenye maji machafu yanayoaminika kuchotwa ndani ya Mto Nairobi ambao umegeuka ‘jaa’ la kila aina ya takataka.

Kwa mujibu wa ripoti, mwanaume huyo aliokota barakoa zilizotumika karibu na hospitali ya Mbagathi jijini Nairobi, ambapo wagonjwa wa virusi vya corona wanatibiwa, na kwenda kuzisafisha kabla ya kuziuza tena jijini Nairobi.

Wakenya, haswa katika vitongoji duni jijini Nairobi, sasa wanahofia kuwa huenda baadhi ya barakoa zinazouzwa mitaani zikawafanya kuambukizwa virusi vya corona badala ya kuwakinga.

Uchunguzi uliofanywa na Taifa Leo katika mitaa ya Mathare, Kibera na Mukuru kwa Njenga jijini Nairobi, ulibaini kuwa takataka ya barakoa zilizotumika zimetapakaa kila mahali.

Barakoa zilizotumika zinatupwa ovyo hivyo kuwaweka wakazi katika hatari ya kuambukizwa virusi vya corona.

Katika, mtaa wa Kibera, barakoa zilizotumika zimetupwa kando ya barabara na ndani ya Mto Nairobi uliosheheni takataka

Lakini Bw Jack Omondi ambaye ni mkazi wa Kibera anasema kuwa wengi wanalazimika kutupa barakoa kiholela kutokana na ukosefu wa vyoo na majaa ya takataka.

Kibera na Mathare ni miongoni mwa maeneo jijini Nairobi yaliyo na idadi kubwa ya maambukizi ya virusi vya corona.

Wataalamu wa afya na wanaharakati wanahofia kuwa uchafu wa barakoa na glovu zilizotumika unaweza kuchangia katika kusambaa kwa virusi vya corona.

Shirika la Umoja wa Mataifa kuhusu Mazingira (UN Environment) tayari limeonya kuwa janga la virusi vya corona litasababisha kuongezeka kwa maelfu ya tani za takataka ambazo ni hatari kwa afya na mazingira.

Shirika hilo linasema kuwa takataka hatari zinajumuisha zinajumuisha barakoa, glovu na vifaa vya matibabu vilivyotumiwa katika kuzuia maambukizi ya virusi vya corona.

Ripoti kuhusu Hali ya Uchumi nchini ya 2020 iliyotolewa na Shirika la Takwimu (KNBS) miezi miwili iliyopita inaonyesha kuwa serikali za kaunti tayari zimelemewa na kiasi kikibwa cha takataka zinazozalishwa katika miji mbalimbali nchini.

Jijini Nairobi, kwa mfano, kiasi cha takataka kiliongezeka mwaka jana kutoka tani milioni 2.7 mnamo 2018 hadi tani milioni 2.9.

Serikali ya Kaunti ya Nairobi ilifanikiwa kuzoa asilimia 55.3 ya takataka hizo na kuacha asilimia 45.7 ya uchafu umetapakaa mitaani.

Kati ya tani 320,000 za takataka zilizozalishwa jijini Mombasa mwaka jana ni tani 147,000 tu zilizokusanywa na serikali ya kaunti.

Serikali ya Kaunti ya Kisumu ilifanikiwa kuzoa tani 63,000 tu kati ya tani 210,000 za uchafu uliozalishwa jijini humo.

Kuna hofu kuwa takataka za barakoa zilizotumika huenda zikasababisha ongezeko la maambukizi ya virusi vya corona nchini huku mitaa ya mabanda ikitarajiwa kuathirika zaidi.

Ripoti ya sensa ya 2019, inaonyesha kuwa mitaa ya mabanda inaongoza kwa kutupa takataka kiholela bila kuzingatia kanuni za usafi.

Asilimia 42.6 ya wakazi wa mtaa wa Kibra, ambao unaongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya maambukizi ya virusi vya corona jijini Nairobi, hutupa takataka barabarani, mitaroni au vyanzo vya maji, kulingana na ripoti ya sensa ya 2019.

Asilimia 20.1 na asilimia 15.1 ya wakazi wa mtaa wa Mathare na Starehe mtawalia hutupa takataka zao za nyumbani kiholela katika vyanzo vya maji, mitaro ya kupitisha maji taka na barabarani.

Ripoti ya Sensa inaonyesha kuwa asilimia 7.8 ya familia milioni 1.5 zilizoko jijini Nairobi hutupa takataka za nyumbani ovyo ovyo barabarani na mitaroni. Familia hizo ndizo huchangia kwa kiasi kikubwa katika uchafuzi wa Mto Nairobi.

Ripoti hiyo pia inaonyesha kuwa takribani familia 20,000 jijini Mombasa zinatupa takataka za nyumbani kiholela.

Nchini Kenya, kulingana na ripoti ya sense ya 2019, kuna jumla ya kaya milioni 12 lakini ni asilimia 6.3 tu ambazo takataka zao huzolewa na serikali za kaunti.

Katibu mkuu wa shirika la kutetea mazingira la United Green Movement, Hamisa Zaja, anasema kuwa utupaji ovyo wa barakoa na mavazi mengineyo ya kukinga virusi vya corona kunaweza kusababisha maradhi hayo kusambaa zaidi, haswa katika maeneo yenye msongamano mkubwa wa watu.

Bi Zaja anasema idadi kubwa ya Wakenya hawana ufahamu kuhusu njia salama za kutupa barakoa, glovu au mavazi mengineyo ya kuwakinga dhidi ya kuambukizwa virusi vya corona.

“Wakati huu wa janga la virusi vya corona, idadi kubwa ya Wakenya wanatumia barakoa na glovu kujikinga dhidi ya maambukizi. Lakini baada ya kuzitumia hawajui mahali pa kupeleka takataka hizo,” anasema.

Bi Zaja anaitaka serikali kuimarisha juhudi za kuwaelimisha Wakenya kuhusu njia mwafaka za kutupa uchafu unaotokana na vifaa au mavazi ya kuzuia maambukizi ya virusi vya corona.

James Wambugu ambaye ni muuzaji wa barakoa mtaani Mukuru kwa Njenga anasema kwamba amekuwa akijaribu kuwaelimisha wateja wake kuhusu njia mwafaka za kutupa barakoa zilizotumika lakini wengi wao wanapuuzilia mbali ushauri wake.

“Serikali inafaa kuhamasisha umma kuhusu jinsi ya kukusanya uchafu wa barakoa ili usije ukaambukiza zaidi virusi vya corona,” anasema.

Tafiti ambazo zimefanywa zinaonyesha kuwa idadi kubwa ya Wakenya wanaamini kuwa kuvalia barakoa ni njia mojawapo ya kuzuia maambukizi ya virusi vya corona.

Utafiti uliofanywa na KNBS mwezi uliopita ulionyesha kuwa asilimia 79 ya Wakenya wanaamini kuwa wakivalia barakoa wanazuia kusambaa kwa virusi vya corona.

Utafiti uliofanywa na shirika la TIFA katika mitaa duni jijini Mombasa na Nairobi pia ulionyesha kuwa asilimia 3 ya Wakenya wanaamini kuwa kuvalia glovu kunawakinga dhidi ya virusi vya corona.

Mwongozo

Katibu wa Wizara ya Mazingira na Misitu Chris Kiptoo anasema kuwa wananchi wanafaa kufuata mwongozo wa Mamlaka ya Uhifadhi wa Mazingira (Nema) kuhusu njia mwafaka za kutupa barakoa au vifaa vya kujikinga na virusi vya corona.

Dkt Kiptoo anasema kuwa utupaji kiholela barakoa au vifaa vinginevyo vya kimatibabu ni hatari kwa mazingira na afya ya binadamu.

Waziri wa Afya Mutahi Kagwe mnamo Aprili alikiri kuwa kuna changamoto ya utupaji takataka kuhusu utupaji wa vifaa ya kujikinga na virusi vya corona kama vile barakoa na glovu.

Bw Kagwe, hata hivyo, alisema kuwa serikali imeandaa mwongozo kuhusu njia salama za kutupa takataka hizo bila kuhatarisha mazingira na afya ya watu.

Mkurugenzi Mtendaji wa Nema Mamo Mamo anasema kuwa uchafu wa barakoa na glovu ni miongoni mwa takataka zilizowekwa kwenye kundi la ‘uchafu hatari wa hospitalini’.

“Asilimia 85 ya takataka zinazotokana na vifaa vya kimatibabu huwa hazina madhara. Lakini asilimia 15 ni hatari kwa afya kwani zinaweza kuwa na virusi, bakteria, sumu na hata zinaweza kulipuka,”anasema Bw Mamo.

“Baadhi ya vifaa vya kujikinga na virusi vya corona kama vile barakoa na glovu hutumika mara moja na kisha kutupwa. Hali hiyo imesababisha ongezeko la takataka nchini. Iwapo hatua za haraka hazitachukuliwa basi huenda kukawa na maambukizi zaidi ya virusi vya corona na uchafuzi wa mazingira,” anaongezea.

Anasema kuwa barakoa, glovu na vifaa vinginevyo vya kujikinga na virusi vya corona vinajumuishwa katika kundi la takataka za hospitalini hivyo unafaa kutupwa kwa mujibu wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya 1999.

Kulingana na mwongozo wa Nema; barakoa, glovu, chupa za sabuni na dawa ya kuua viini (sanitaiza) hazifai kuchanganywa na takataka nyingine nyumbani.

“Virusi vya corona vinaishi kwa siku nyingi juu ya vitu kama vile barakoa au glovu hivyo unapotupa takataka ndani ya nyumba au njiani, sokoni, nje ya dirisha la matatu, nakadhalika, unahatarisha maisha yaw engine,” anasema Bw Mamo.

Mkurugenzi wa Nema, hata hivyo, anakiri kuwa idadi kubwa ya Wakenya hawana mazoea ya kutenganisha takataka na wamekuwa wakitupa kiholela.

“Kuchanganya barakoa na takataka nyinginezo za nyumbani kunatia hatarini watu ambao huokota chupa na vitu vingine katika majaa,” anasema.

Mwongozo wa Nema unahitaji wamiliki wa nyumba za kupanga kuweka jaa, linalofunguliwa kwa miguu kuwezesha wapangaji kutupa hapo takataka hatari kama kama vile barakoa zilizotumia.

Matatu na afisi pia zinafaa kuwa na majaa hayo spesheli ya kutupa takataka zinazoweza kusababisha maambukizi ya maradhi, kwa mujibu wa mwongozo wa Nema.

Katika maeneo ya vijijini, mwongozo wa Nema unahitaji serikali za kaunti kusambaza majaa ya kukusanya takataka zinazoweza kusababish maambukizi katika afisi za machifu, sokoni au eneo lolote linaloweza kufikiwa na watu wengi.

Bw Mamo anasema kuwa nyumbani, haswa katika maeneo ya vijijini, takataka zilizo na barakoa zinafaa kunyunyuziwa kemikali ya Sodium hypochlorite na kisha kutumbukizwa kwenye shimo la choo.

Ripoti ya Sensa inaonyesha kuwa asilimia 3.6 ya familia, ambazo ni sawa na familia 434,000, kote nchini hutupa takataka ndani ya shimo la choo.

Marufuku

Serikali mnamo Aprili ilipiga marufuku watu kuabiri magari ya umma, kwenda madukani, sokoni au kuabiri bodaboda bila kuvalia barakoa.

Mtu anayepatikana na hatia ya kuvunja sheria hiyo anatozwa faini ya Sh20,000 au kifungo cha miezi sita gerezani.

Barakoa zimejizolea umaarufu kutoka na ukweli kwamba zimesaidia kupunguza maambukizi ya virusi vya corona kote duniani.

Shirika la WHO linasema kuwa watu wanapozungumza, kukohoa, kuchemua au kucheka wanatoa mate ambayo yanaweza kuwa na virusi vya corona ambavyo husalia hewani kwa muda mrefu.

Shirika la WHO linapendekeza kuwa watu wasio na barakoa watumie katarasi shashi au kitambaa wanachoweza kutupa mara baada ya kukohoa au kuchemua.

Watu ambao hawajavalia barakoa wanapoenda katika eneo lililo na virusi vya corona hewani wanaambukizwa bila hata baada ya waathiriwa kuondoka.

Hiyo ndiyo maana serikali sasa inataka kila mtu anayeenda nje ya nyumba yake kuvalia maski ili kujikinga.

Tafiti zilizofanywa zinaonyesha kuwa ni vigumu kuambukizwa virusi vya corona iwapo utatangamana na mwathiriwa ikiwa wote mmevalia barakoa.

You can share this post!

Corona yasababisha mfadhaiko katika jamii

Handisheki yageuza ‘Baba’ bubu

adminleo