• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 1:14 PM
Madiwani sasa watishia kumtimua Joho

Madiwani sasa watishia kumtimua Joho

Na FARHIYA HUSSEIN

BAADHI ya madiwani wa Kaunti ya Mombasa, wametishia kumtimua ofisini Gavana Hassan Joho, wakimlaumu kwa ufisadi na kuwadharau.

Haya yanajiri siku chache baada ya madiwani hao kumshtaki Bw Joho kwa Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC), wakitaka achunguzwe kwa madai ya matumizi mabaya ya pesa.

Diwani wa wadi ya Jomvu Kuu, Bw Athman Shebe, alisema kwamba wanatumia sheria kumuondoa Bw Joho ofisini.

Hata hivyo, wanaomuunga Bw Joho walipuuza tisho hilo wakisema wanaolalamika hawana idadi ya kutosha kufanikisha mswada wa kumuondoa ofisini.

“Iwapo wataweza kuwasilisha mswada katika bunge la kaunti, watahitaji kuuungwa na theluthi mbili ya wawakilishi,” alisema diwani wa Likoni, Bw Athman Mwamiri.

Alisema ili mswada wao uweze kukubaliwa, watahitajika kukusanya sahihi za madiwani 14.Bw Shebe alisema kwamba madiwani wengi wanaunga mkono kutimuliwa kwa Joho japo wanaogopa kutamka hadharani.

“Wawakilishi wengi wa wadi wanaogopa kuonekana ama kusikika hadharani wanataka kumuondoa gavana. Hii ndio sababu kuu ya sisi kufuata njia za kisheria na tayari tumeanza kukusanya sahihi,” akasema Bw Shebe.

Mwenyekiti wa Chama cha ODM kaunti ya Mombasa, Bw Mohammed Hatimy, ambaye anasimamia fedha katika kaunti ya Mombasa, alisema kwamba Bw Joho yuko tayari kujitetea kortini.

“Ikiwa ni kweli wana ushahidi, basi wauwasilishe. Pesa wanazotushtumu kwa matumizi mabaya zilitumika kuwalipa wafanyakazi mshahara, kumaliza miradi, na baadhi ya maswala mengine,” alisema.

Madiwani Bw Charles Kitula (Freretown), Athman Shebe (Jomvu Kuu), Abarari Omar (Kongowea), Fahad Kassim (Mjambere) ni miongoni mwa wanaotaka Bw Joho kuondolewa ofisini.

Wanne hao walipokonywa nyadhifa za uongozi katika bunge la kaunti kwa kumshtaki Bw Joho kwa EACC.

You can share this post!

Ageuza shule kuwa karakana

Safiri salama ‘Papa’, tutaonana baadaye

adminleo