• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 9:50 AM
Mbio za Kip Keino Classic sasa zaahirishwa kutoka Septemba 26 hadi Oktoba 3, 2020

Mbio za Kip Keino Classic sasa zaahirishwa kutoka Septemba 26 hadi Oktoba 3, 2020

Na CHRIS ADUNGO

MBIO za kimataifa za Kip Keino Classic zilizokuwa ziandaliwe katika uwanja wa kitaifa wa Nyayo, Nairobi mnamo Septemba 26, 2020, sasa zimeahirishwa hadi Oktoba 3, 2020.

Kuratibiwa upya kwa mbio hizo kunachochewa na

mabadiliko kwenye ratiba ya mashindano mbalimbali ya riadha.

Kivumbi cha Diamond League kilichokuwa kifanyike jijini Doha, Qatar mnamo Oktoba sasa kitatifuliwa Septemba 26, siku ambapo mbio za Kip Keino Classic zilikuwa zimepangiwa pia kunogeshwa.

Riadha za Kip Keino Classic zitaandaliwa sasa siku moja kabla ya Mkenya Eliud Kipchoge na Kenenisa Bekele wa Ethiopia kunogesha mbio za London Marathon.

Kipchoge na Bekele ni miongoni mwa wanariadha 40 wa haiba kubwa zaidi duniani watakaoshiriki kivumbi cha London Marathon ambacho kwa kawaida huvutia zaidi ya watimkaji 40,000.

Kip Keino Classic ni miongoni mwa duru za kivumbi cha World Athletics Continental Tour kilichofunguliwa rasmi jijini Turku, Finland mnamo Agosti 11, 2020.

Kipute cha Turku kilipewa jina Paavo Nurmi kwa heshima ya aliyekuwa mwanariadha nguli wa taifa hilo, Nurmi ambaye alijinyakulia medali tisa za dhahabu na tatu za fedha katika fani mbalimbali za Olimpiki zilizoandaliwa 1920 (Antwerp, Ubelgiji), 1924 (Paris, Ufaransa) na 1928 (Amsterdam, Uholanzi).

Mbio za Continental Tour zitashirikisha nyingi za fani ambazo zimeondolewa kwenye kivumbi cha Diamond League msimu huu wa 2020 zikiwemo mbio za mita 200 na mita 3,000 kuruka viunzi na maji.

Makala ya kwanza ya Continental Tour yalikuwa yafanyike humu nchini mnamo Mei 2, 2020 ila yakaahirishwa kutokana na ugonjwa wa Covid-19.

Licha ya duru nzima kuitwa Kip Keino Classic kwa heshima ya mwanariadha veterani Kipchoge Keino, kivumbi cha fani ya mbio za mita 10,000 wakati wa mashindano hayo kitaitwa “Naftali Temu 10,000m Classic”.

Kipchoge alijizolea nishani ya dhahabu katika mbio za mita 1,500 kwenye Olimpiki za 1968 nchini Mexico kabla ya kutwaa medali nyingine ya dhahabu katika mbio za mita 3,000 kuruka viunzi na maji kwenye Olimpiki za 1972 jijini Munich, Ujerumani.

Kwa upande wake, Temu alitwalia Kenya nishani ya kwanza na ya mwisho katika mbio za mita 10,000 kwenye Olimpiki mnamo 1968 nchini Mexico. Kipchoge, Temu na Amos Biwott (mita 3,000 kuruka viunzi na maji), ndio Wakenya wa kwanza kunyakua medali za dhahabu kwenye Michezo ya Olimpiki mnamo 1968 nchini Mexico.

“Kipchoge ndiye baba wa Riadha za Kenya na dunia nzima inamfahamu zaidi kuliko Mkenya yeyote mwingine katika ulingo wa riadha,” akasema Mwenyekiti wa Shirikisho la Riadha la Kenya (AK) tawi la Nairobi, Barnaba Korir kwa kusisitiza kwamba kuita mbio za mita 10,000 ‘Naftali Temu’ kutachochea zaidi Wakenya kutamba katika fani hiyo wakati wa Olimpiki zijazo jijini Tokyo, Japan.

Mwingereza Mo Farah na Waethiopia ndio wamekuwa wakitawala mbio za mita 10,000 duniani kwa kipindi kirefu kilichopita.

RATIBA YA CONTINENTAL TOUR:

• Paavo Nurmi Games (Turku, Finland, Agosti 11);

• Istvan Gyulai Memorial (Szekesfehervar, Hungary, Agosti 19);

• Seiko Golden Grand Prix (Tokyo, Japan, Agosti 23);

• Kamila Skolimowska Memorial (Silesia, Poland, Septemba 6);

• Ostrava Golden Spike (Ostrava, Czech, Septemba 8);

• Memorial Borisa Hanzekivica (Zagreb, Croatia, Septemba 15);

• Kip Keino Classic (Nairobi, Kenya, Oktoba 3)

• Nanjing Continental Tour (Nanjing, China, tarehe bado haijathibitishwa).

You can share this post!

SRC yapinga pensheni ya wabunge

Blaise Matuidi asajiliwa rasmi na Inter Miami ya Amerika