• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Hatua kwa hatua, Simbas wajinyanyua viwango vya raga

Hatua kwa hatua, Simbas wajinyanyua viwango vya raga

Na GEOFFREY ANENE

KWA wiki ya pili mfululizo, Kenya imeimarika katika viwango bora vya raga ya wachezaji 15 kila upande duniani bila kuteremka uwanjani.

Katika viwango vipya ambavyo Shirikisho la Raga duniani (World Rugby) imetangaza Jumatatu, Simbas, timu ya Kenya inavyofahamika kwa jina la utani, imeruka juu nafasi moja hadi nambari 29.

Vijana wa kocha Ian Snook waliimarika kutoka nafasi ya 31 hadi 30 hapo Mei 7 baada ya Chile kulazwa 28-12 na Brazil katika Kombe la Amerika Kusini mnamo Mei 5. Wameimarika tena kutokana na Korea Kusini kupepetwa 30-21 na Hong Kong katika Kombe la Bara Asia hapo Mei 12.

Simbas haijacheza mechi ya kimataifa tangu ziara yake ya Hong Kong mwezi Novemba mwaka 2017. Itafungua mwaka 2018 dhidi ya majirani na mahasimu wa jadi Uganda katika Kombe la Elgon hapo Mei 26 jijini Kampala. Vijana wa Snook wanatarajiwa kuingia kambini Mei 18 katika eneo la Nanyuki.

New Zealand, Jamhuri ya Ireland, Uingereza, Australia, Scotland, Afrika Kusini, Wales, Ufaransa, Argentina na Fiji zinashikilia katika nafasi 10 za kwanza duniani, mtawalia. Zimesalia katika nafasi hizo.

Mabingwa wa Afrika, Namibia wamesalia katika nafasi ya 24 duniani. Namibia inashikilia nafasi ya kwanza Afrika baada ya Afrika Kusini, ambayo haishiriki Kombe la Dhahabu la Afrika (Gold Cup).

Kenya inafuata Namibia katika viwango bora vya Afrika, huku Uganda ikisalia katika nafasi ya 34 duniani na nambari tatu Afrika. Morocco imetupwa chini nafasi moja hadi nambari 40 duniani baada ya Paraguay kuzima Colombia 28-26 katika Kombe la Amerika Kusini.

Tunisia imenufaika na Colombia kupoteza. Imepaa nafasi moja hadi nambari 42 duniani. Zimbabwe inasalia katika nafasi ya 44 duniani. Namibia, Kenya, Uganda, Morocco, Tunisia na Zimbabwe zitawania ubingwa wa Kombe la Dhahabu la Afrika mwaka 2018 ambalo litatumika kuchagua mwakilishi wa Afrika katika Kombe la Dunia mwaka 2019.

Ratiba ya Simbas mwaka 2018:

Mei 26 – Uganda vs. Kenya (Elgon Cup, Kampala)

Juni 23 – Morocco vs. Kenya (Africa Gold Cup, Casablanca)

Juni 30 – Kenya vs. Zimbabwe (Africa Gold Cup, Nairobi)

Julai 7 – Kenya vs. Uganda (Africa Gold Cup, Nairobi)

Agosti 11 – Kenya vs. Tunisia (Africa Gold Cup, Nairobi)

Agosti 18 – Namibia vs. Kenya (Africa Gold Cup, Windhoek)

Kikosi cha Simbas: Patrick Ouko (Homeboyz), Oscar Simiyu (KCB), Moses Amusala (KCB), Joseph Odero (Kabras), Nelson Nyandat (KCB), Curtis Lilako (KCB), Peter Karia, (KCB), Phillip Ikambilli, (Homeboyz), Coleman Were (Kabras), Oliver Mangeni (KCB),Malcolm Onsando (Quins),Eric Kerre (Impala),Wilson Kopondo, (Quins),Andrew Chogo (Kabras),George Nyambua (Kabras), Dalmus Chituyi (Homeboyz), Peter Misango (Quins), Elkeans Musonye (Strathmore), Martin Owila (KCB), Davis Chenge (KCB),  Samson Onsomu (Impala), Xavier Kipng’etich (Impala), Mohammed Omollo (Homeboyz),Isaac Adimo (Quins), Biko Adema (Nondies), Leo Seje (Impala), Maxwell Kangeri (Homeboyz), Peter Kilonzo (KCB), Zedden Marrow (Homeboyz), Tony Onyango (Homeboyz),Felix Ayange (Kabras), Jacob Ojee (KCB), Darwin Mukidza (KCB), Edmund Anya (Strathmore),Vincent Mose (Impala).

You can share this post!

USM Alger yatua nchini kukabiliana na Gor Confederations Cup

Afrika Kusini wajiondoa kwa kipute cha raga ya wanawake...

adminleo