• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
‘Tangatanga’ wasihi Uhuru azungumze na Ruto

‘Tangatanga’ wasihi Uhuru azungumze na Ruto

Na ONYANGO K’ONYANGO

WANDANI wa Naibu Rais William Ruto wamemsihi Rais Uhuru Kenyatta afanye mazungumzo na naibu wake ili kumaliza uhasama uliopo baina ya viongozi hao.

Viongozi hao wamemtaka Rais Kenyatta na Dkt Ruto wapatane ili kumaliza tofauti baina yao ambazo zimesababisha chama cha Jubilee kugawanyika.

Akizungumza katika eneo la Kamukunji, Eldoret, katika Kaunti ya Uasin Gishu, Naibu Katibu Mkuu wa Jubilee Caleb Kositany alimtaka Rais Kenyatta na Naibu wake William Ruto wapatane ili kutuliza joto la kisiasa ambalo limeanza kushuhudiwa humu nchini.

“Jinsi tulivyokuwa tukipanga mwaka wa 2013 kuhusu ni nani alifaa kuwa Rais na naibu, kisha wawili hao wakakubali kukaa pamoja, ndivyo wanavyofaa wazungumze kisha watupe mwelekeo kama wafuasi wa Jubilee ili tukomeshe haya mambo tunayoshuhudia,” akasema Bw Kositany.

Alikuwa ameandamana na Mbunge wa Bahati Kimani Ngunjiri ambaye alimwondolea lawama Dkt Ruto kutokana na matamshi yaliyotolewa na Bw Ng’eno na Bw Sudi.

Lakini kwa mujibu wa mbunge wa Nyeri Mjini Wambugu Ngunjiri ambaye anaegemea mrengo wa Rais Kenyatta, Dkt Ruto anafaa kujilaumu kwa kusababisha uhasama wa kisiasa baina yake na kiongozi wa nchi.

Bw Ngunjiri alisema kuwa Rais Kenyatta alikuwa ameahidi Dkt Ruto kwamba angempigia debe katika kinyang’anyiro cha urais 2022 iwapo asingefanya kampeni za mapema.

Bw Ngunjiri alisema kuwa kitumbua cha Naibu Rais kiliingia mchanga alipopinga Mpango wa Maridhiano (BBI) ambao Rais Kenyatta anataka kutumia kuacha taifa likuwa limeungana atakapostaafu 2022.

“Rais aliweka wazi kuwa hataweza kufanikisha ndoto yake ya kuunganisha taifa hili iwapo kutakuwa na kampeni za mapema. Kampeni hugawanya watu na hiyo ndiyo maana Rais amekuwa akipinga siasa za mapema,”

“Inashangaza kuwa Naibu wa Rais alianza mchakato wa kutaka kumrithi Rais Kenyatta mara tu baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2017 uliokuwa umegawanya taifa hili,” akasema Bw Wambugu.

You can share this post!

Naomi Osaka ana hela za kukausha bahari licha ya umri mdogo

Mbona amri za Uhuru zapuuzwa?