• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 9:50 AM
Messi ahisi Suarez alinyimwa fursa ya kuondoka Barcelona kishujaa

Messi ahisi Suarez alinyimwa fursa ya kuondoka Barcelona kishujaa

Na MASHIRIKA

LIONEL Messi alitumia mtandao wake wa Instagram kumuaga rasmi rafikiye Luis Suarez ambaye aliondoka Barcelona kwa wingi wa machozi mnamo Septemba 24, 2020, na kutua Atletico Madrid ya Uhispania waliompa mkataba wa miaka miwili.

“Leo nilienda kwenye chumba cha kubadilishia sare na ukweli kwamba sitacheza pamoja na Suarez msimu huu ukanibainikia,” akasema Messi kabla ya kukashifu usimamizi wa Barcelona kwa mara nyingine.

“Suarez, ulistahili kuondoka Camp Nou kwa hadhi. Ulikuwa miongoni mwa wanasoka muhimu na tegemeo kubwa katika historia ya Barcelona,” akaendelea Messi.

“Hukustahili kabisa kutimuliwa Barcelona kwa namna ulivyofanyiwa.”

“Ukweli ni kwamba kufikia sasa, hakuna jingine kubwa linalonishangaza zaidi,” akasema mfumaji na nahodha huyo wa Barcelona na timu ya taifa ya Argentina.

Mbali na Suarez, 33, rafiki mwingine mkubwa wa Messi uwanjani Camp Nou, Arturo Vidal ameondoka Barcelona na kutua Inter Milan kuungana na kocha wake wa zamani kambini mwa Juventus, Antonio Conte.

Suarez alijiunga na Barcelona mnamo 2014 baada ya kuagana na Liverpool kwa kima cha Sh10.3 bilioni. Tangu wakati huo, ameshindia Barcelona mataji manne ya La Liga, manne ya Copa del Rey, moja la UEFA na jingine la Kombe la Dunia mnamo 2015. Aliwafungia Barcelona jumla ya mabao 198 kutokana na mechi 283 katika kipindi cha miaka sita.

Wakiwa Barcelona, Messi na Suarez walikuwa majirani katika mtaa wa kifahari wa Castelldefels viungani mwa jiji la Barcelona na walikuwa na mazoea ya kuondoka na kuwasili pamoja uwanjani Camp Nou kwa mazoezi.

Rais wa Barcelona, Josep Maria Bartomeu anatazamiwa sasa kuondoka mamlakani baada ya kampeni ya kupigwa kwa kura ya kutokuwa na imani naye kupata uungwaji mkono miongoni mwa wadau wa kikosi hicho cha La Liga.

Bartomeu alichaguliwa kuwa Rais wa Barcelona mnamo 2014 na uongozi wake umekashifiwa pakubwa kiasi cha kuhusishwa na maamuzi ya hivi karibuni ya Messi kutaka kuondoka ugani Camp Nou.

Mpango wa kuondolewa kwa Bartomeu kupitia kura ya maoni ulifichuliwa na vinara wa Barcelona siku moja baada ya Messi kuwasilisha barua ya kutaka kuachiliwa kuondoka Camp Nou.

Kufikia sasa, saini 20,731 kutoka kwa mashabiki na wasimamizi wa Barcelona wanaounga mkono mpango huo zimepatikana, kumaanisha kwamba Bartomeu yuko pua na mdomo kuondolewa mamlakani kupitia kura ya wadau kutokuwa na imani naye.

Ili kufanikisha maandalizi ya kura hiyo, jumla ya saini 16,500 pekee ndizo zilizohitajika kuwasilishwa na kukaguliwa na wahusika kabla ya Bartomeu, 57, kuondolewa kupitia refarenda chini ya kipindi cha miezi mitatu ijayo.

Refarenda ya kumng’atua Bartomeu itashuhudia wanachama 150,000 wa Barcelona wakipiga kura na iwapo asilimia 66.5 ya wanachama watapiga kura ya kumwondoa, basi uongozi wake utafikia kikomo.

Bartomeu alitarajiwa kukamilisha rasmi kipindi chake cha uongozi cha mihula miwili mnamo Machi 2021.

Iwapo kura ya kutokuwa na imani naye itaandaliwa, basi atakuwa rais wa tatu wa Barcelona kuondolewa mamlakani kwa jaribio la njia hiyo baada ya Josep Lluis Nunez mnamo 1998 na Joan Laporta mnamo 2008. Mpango wa kung’atuliwa kwa wawili hao kupitia refarenda miaka hiyo haukufaulu.

Messi aliyekuwa akiwaniwa pakubwa na Manchester City ya Uingereza, alihiaria kusalia Barcelona japo huenda akabanduka rasmi baada ya mkataba wake kutamatika mwishoni mwa 2020-21.

Chini ya urais wa Bartomeu, Barcelona wamekabiliwa na visa vya matumizi mabaya ya fedha na kikosi hicho kilikamilisha kampeni za msimu huu bila kutwaa taji lolote kwa mara ya kwanza tangu 2008.

Walibanduliwa mapema na Athletic Bilbao kwenye Copa del Rey, wakapigwa kumbo na Real Madrid kwenye La Liga na kudhalilishwa na Bayern Munich kwa kichapo cha 8-2 kwenye robo-fainali za Klabu Bingwa Ulaya (UEFA).

You can share this post!

Msiogope kutukosoa, Rais aambia viongozi wa kidini nchini

Ndidi kukosa mechi za Leicester kwa wiki 12 kutokana na...