• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 5:55 AM
#KipKeinoClassic:  Paul Tanui ashinda mbio za mita 10,000

#KipKeinoClassic: Paul Tanui ashinda mbio za mita 10,000

Na GEOFFREY ANENE

NYOTA Paul Tanui ndiye mshindi wa makala ya kwanza ya mbio za mita 10,000 za kitaifa kwenye Riadha za Dunia za Continental Tour za Kip Keino Classic zinazoendelea katika uwanja wa Nyayo mnamo Oktoba 3, 2020.

Tanui,29, ambaye aliridhika na medali ya fedha nyuma ya Muingereza Mo Farah katika mbio hizi za mizunguko 25 kwenye Michezo ya Olimpiki 2016 mjini Rio de Janeiro nchini Brazil, alisubiri hadi ikisalia mizunguko miwili alipochomoka kama risasi na kutwaa taji la Kip Keino Classic kwa dakika 28:06:91.

Mshindi huyu wa medali za shaba kwenye Riadha za Dunia mwaka 2013 mjini Moscow nchini Urusi, 2015 mjini Beijing nchini Uchina na 2017 mjini London nchini Uingereza, alifuatwa kwa karibu na Nathan Lagat na mshindi wa medali ya fedha ya mbio za kilomita 21 kwenye Michezo ya Bara Afrika ya Ufukweni 2019 Charles Yosei Mneria.

Rhonex Kipruto, ambaye aliweka rekodi ya dunia ya mbio za kilomita 10 kwa wakimbiaji wasiozidi umri wa miaka 20 ya dakika 26:24 hapo Januari 12 mwaka huu mjini Valencia, alikuwa amepigiwa upatu wa kung’arA katika kitengo hiki kichovutia wakimbiaji 25. Hata hivyo, Kipruto,20, ambaye anapanga kujitosa katika mbio za kilomita 21 kwa mara ya kwanza kabisa hapo Desemba 6 mjini Valencia, alikamilisha katika nafasi ya nne.

Naye William Mbevi ameshinda mbio za mita 400 kuruka viunzi kwa sekunde 51:30 akifuatwa unyounyo na Nicholas Chirchir (51:48) na Edward Ngunjiri (51:91).

You can share this post!

#KipKeinoClassic: Vanice Kerubo aibuka mshindi wa mbio za...

David Ndii: Si dhambi kushirikiana na Ruto kutwaa urais 2022