• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 2:25 PM
Kiprotich aapa kumaliza utawala wa Julius Yego

Kiprotich aapa kumaliza utawala wa Julius Yego

Na GEOFFREY ANENE

“Hapa ni nyumbani kwetu na ilikuwa lazima tulinde.” Huo ndio ujumbe wa mrushaji mkuki Alexander Toroitich Kiprotich baada ya kushindia Kenya medali ya dhahabu katika fani ya uwanjani ya kurusha mkuki kwenye riadha za Kip Keino Classic uwanjani Nyayo jijini Nairobi, Jumamosi.

Kiprotich, ambaye mtupo wake bora ni mita 78.84 alioandikisha mjini Eldoret mwaka 2015, alibeba taji baada ya kurusha mkuki umbali wa mita 76.71.

“Nimejawa na ari ya kujiondoa kutoka kivuli cha bingwa wa dunia wa mwaka 2015 Julius Yego baada ya kumaliza nyuma yake kwa muda mrefu sana. Kwa kushinda makala ya kwanza ya Kip Keino Classic ni kitu cha kihistoria na ninatumai kutetea taji langu katika makala ya pili mwezi Mei 2021,” aliongeza Kiprotich, ambaye atagonga umri wa miaka 26 hapo Oktoba 10.

Kiprotich alifuatwa katika nafasi ya pili na Hubert Chmielak kutoka Poland (mita 75.47) na Timothy Herman kutoka Ubelgiji (75.18).

Warushaji mkuki kutoka Kenya, Poland, Ubelgiji, Jamhuri ya Czech na Ufaransa walishiriki kitengo hiki. Yego, ambaye anashikilia rekodi ya Kenya na Bara Afrika baada ya kurusha mkuki mita 92.72 akishinda taji la dunia mwaka 2015 nchini Uchina, hakushiriki.

You can share this post!

Muethiopia Lemlem aonyesha kinadada Wakenya kivumbi mbio za...

Maafisa waliolinda mlingoti wa Safaricom wajeruhiwa na...