• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 11:38 AM
Simanzi vijana watano marafiki wakiangamia ajalini

Simanzi vijana watano marafiki wakiangamia ajalini

Na Mwangi Muiruri

HALI ya majonzi imetanda katika kijiji cha Kagurumo, Muthithi Kaunti ya Murang’a, baada ya vijana watano marafiki kufariki pamoja kwenye ajali ya pikipiki.

Wakazi wa kijiji hicho wasema bado wamo kwenye hali ya mshtuko kufuatia tukio hilo la Oktoba 25, ambapo mabarobaro hao waliokuwa wamealikwa na mwenzao kusherehekea hatua yake ya kupata pikipiki kufanyia kazi ya bodaboda waliangamia.

Waliofariki kwenye ajali hiyo walitambuliwa kama Samuel Chege, 25, Moses Kamande, 21, James Wanyoike, 25, Duncan Muchiri, 33, na mtu mwingine ambaye hakutambuliwa.

Inadaiwa kuwa siku hiyo, Bw Chege alienda katika kituo cha kibiashara cha Kamucii, na kufanikiwa kupata pikipiki, ambapo angeajiriwa na mwenyewe kama kibarua, kwa kuwabeba watu na kumlipa baadaye.

Kutokana na furaha aliyokuwa nayo, aliwaalika wenzake ‘kuifanyia majaribio’ pikipiki hiyo na kusherehekea mafanikio hayo.Kama sehemu ya ‘sherehe’ hizo, walipanda pikipiki kuelekea katika kituo hicho cha kibiashara.

Hii ni licha ya kanuni za serikali kuhitaji pikipiki kuwabeba watu wawili pekee; dereva na abiria wake.Inadaiwa watano hao walifariki mwendo wa saa sita usiku, pikipiki hiyo ilipogongana na lori katika eneo la Makenji.Cha kusikitisha ni kuwa wakati wa ajali hiyo, wote walikuwa walevi.

 

You can share this post!

Kenya hatarini kunyimwa mikopo kufuatia deni la Sh7 trilioni

Corona na ICC zimemtoa pumzi Ruto – Wadadisi