• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 12:30 PM
Jaji akomesha utata kwa kuwapa wajane ng’ombe

Jaji akomesha utata kwa kuwapa wajane ng’ombe

Na BRIAN OCHARO

MAHAKAMA Kuu ya Malindi, Kaunti ya Kilifi imewapa wajane sita ng’ombe wanne kila mmoja baada ya familia kushindwa kukubaliana kuhusu ugavi wa mifugo hao.

Bw Arthur Jeremiah Tsumah ambaye alikuwa na wake sita na watoto 67, alifariki bila kuacha wasia mnamo 2012.

Baada ya kifo chake familia hiyo ililishindwa kukubaliana jinsi ya kugawana ng’ombe 25 wenye thamani ya Sh720,000 aliowacha marehemu.

Ingawaje familia hiyo ilikuwa na makubaliano ya jinsi ya kugawana mali nyingine ikiwemo mashamba makubwa, nyumba za makazi na za kukodisha zote zikikisiwa kuwa na thamani ya Sh30 milioni, walitofautiana katika ugavi wa mifugo.

Jaji Reuben Nyakundi, ambaye alisimamia suala hilo, aliwafungia watoto wao nje kwa sababu ya idadi yao kubwa na akaamua kugawa mifugo bila kujali idadi ya watoto katika kila nyumba.

Familia hiyo ilitaka kila mmoja wa wajane hao apate sehemu sawa ya mali bila ubaguzi.

Wajane wakubaliane

Ni kwa msingi huu ambapo Jaji alibaini kuwa, suala tata la mifugo liamuliwe baina ya wajane hao bila kuhusisha watoto wao.

“Kwa hivyo kila mwanamke atapewa ng’ombe wanne na watakaobaki wauzwe na mapato wagawiwe kwa usawa,” alisema Jaji.

Jaji pia amethibitisha barua za usimamizi zilizotolewa kwa wasimamizi wa mali hiyo na kuamuru kwamba mali ya mwendazake igawanywe kulingana na makubaliano ya ugavi huo.

“Kwa kuwa huu ni mzozo wa kifamilia hakuna amri yoyote kuhusu gharama ya kesi inatolewa katika uamuzi huu,” alisema jaji.

Korti ilibaini kuwa ushahidi uliotolewa awali kuhusu ugavi ulionyesha kuwa wasimamizi wa mali walikuwa na utata kwa sababu ya kulenga kuwaridhisha wahusika wote.

“Kwa hivyo mahakama haina sababu za kuvuruga jinsi ugavi wa mali ulivyopendezwa isipokuwa mzozo kuhusu mifugo. Jukumu la mahakama kwa hivyo ni kuhakikisha kuwa vigezo vya ugavi wa mali ambayo ilikuwa na utata vinaweza kufanywa kulingana na Sheria ya Urithi,” alisema jaji.

Jaji Nyakundi alibaini kuwa jukumu la wasimamizi ugavi wa mali ilifuata Kifungu cha 38 cha Sheria ya Urithi.

“Ni uamuzi wangu kwamba barua za usimamizi wa mali hiyo ithibitishwe na mali ya marehemu igawanywe kati ya walengwa kwa usawa na wajane pia wazingatiwe kama ilivyopendekezwa na wasimamizi na idhini husika,” alisema jaji huyo

Katika kuzingatia ugavi wa hisa za mali sawa kati ya watoto hao, korti ilisema kwamba ilikuwa dhahiri kwamba binti za marehemu pia walijumuishwa na kupewa kiwango sawa na wenzao wa kiume.

You can share this post!

Badi kuendelea kuhudhuria vikao vya mawaziri

Wakenya Jeptoo na Kotut wasikitika baada ya mbio za Paris...