• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Real Madrid yadidimiza matumaini ya Inter Milan kusonga mbele kwenye gozi la UEFA

Real Madrid yadidimiza matumaini ya Inter Milan kusonga mbele kwenye gozi la UEFA

Na MASHIRIKA

MATUMAINI ya Inter Milan kutinga hatua ya 16-bora ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) msimu huu yalididimizwa na Real Madrid waliowapokeza kichapo cha 2-0 kwenye mchuano wa Kundi B mnamo Novemba 25, 2020, ugani San Siro, Italia.

Kiungo raia wa Chile, Arturo Vidal alionyeshwa kadi nyekundu na refa Anthony Taylor, hatua iliyoyumbisha kabisa uthabiti wa kikosi cha Inter Milan kinachonolewa na kocha Antonio Conte.

Real waliwekwa uongozini na Eden Hazard kupitia penalti ya dakika ya dakika ya saba kabla ya Achraf Hakimi kujifunga na kufanya mambo kuwa 2-0.

Matokeo hayo yalisaza Inter kwenye mkia wa Kundi B kwa alama mbili nyuma ya Shakhtar Donetsk wanaoshikilia nafasi ya tatu kwa pointi nne. Borussia Monchengladbach ya Ujerumani inashikilia nafasi ya kwanza kundini kwa alama nane, moja zaidi kuliko nambari mbili Real ambao ni mabingwa mara 13 wa taji la UEFA.

Gladbach walifunga mabao matatu ya kipindi cha kwanza na kupaa hadi kileleni mwa Kundi B baada ya kuzamisha chombo cha Donetsk kwa mabao 4-0.

Real walikosa huduma za wanasoka Sergio Ramos na Karim Benzema katika mchuano huo.

Inter hawajasajili ushindi wowote katika kampeni za UEFA msimu huu na sasa wako katika hatari ya kutofuzu kwa hatua ya 16-bora ya kivumbi hicho kwa mara ya kwanza tangu 2011-12.

Ushindi wa pili mfululizo uliosajiliwa na Real dhidi ya Inter mwezi huu Novemba umewaweka karibu na kufuzu kwa hatua ya 16-bora ya UEFA kwa mara ya 25 katika historia.

You can share this post!

AFYA: Ni muhimu kupumzika

Atalanta yaduwaza Liverpool kwenye UEFA ugani Anfield