• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 7:50 AM
Lewandowski aongoza Bayern kupepeta Salzburg 3-1 na kufuzu kwa hatua ya 16-bora UEFA

Lewandowski aongoza Bayern kupepeta Salzburg 3-1 na kufuzu kwa hatua ya 16-bora UEFA

Na MASHIRIKA

ROBERT Lewandowski alifunga bao lake la 71 katika kivumbi cha Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) na kusaidia Bayern Munich kupiga RB Salzburg 3-1 na kufuzu kwa hatua ya 16-bora ya kampeni za msimu huu zikisalia mechi mbili zaidi za kupigwa kwenye hatua ya makundi.

Lewandoski ambaye ni raia wa Poland alifungua ukurasa wa mabao dhidi ya wageni wao Red Bull Salzburg kutoka Austria kunako dakika ya 42 kabla ya chipukizi raia wa Ufaransa, Kingsley Coman kuongeza goli la pili dakika 10 baadaye.

Nyota wa zamani wa Manchester City, Leroy Sane aliongeza bao la tatu kwa upande wa Bayern katika dakika ya 68, sekunde chache baada ya kiungo Marc Roca wa Bayern kuonyeshwa kadi nyekundu katika mchuano wake wa kwanza wa UEFA.

Salzburg walifutiwa machozi na Mergim Berisha aliyemwacha hoi kipa Manuel Neuer katika dakika ya 73.

Chini ya kocha Hansi Flick, Bayern ambao ni mabingwa watetezi wa UEFA kwa sasa wanajivunia kushinda mechi zote nne za Kundi A ambalo pia linajumuisha Atletico Madrid na Lokomotiv Moscow.

Idadi ya mabao ambayo sasa yamefungwa na Lewandowski kwenye kipute cha UEFA inawiana na magoli yanayojivuniwa na nyota wa zamani wa Real Madrid, Raul Gonzalez.

Wawili hao wanashikilia nafasi ya tatu kwenye orodha ya wafungaji bora wa muda wote katika UEFA nyuma ya Lionel Messi wa Barcelona (mabao 118) na Cristiano Ronaldo wa Juventus (mabao 131)

Mbali na Lewandowski, Coman na Sane, mchezaji mwingine aliyeridhisha zaidi kwa upande wa Bayern ni kiungo wa zamani wa Arsenal, Serge Gnabry ambaye alichangia bao la Coman na Sane.

Licha ya kumiliki asilimia kubwa ya mpira katika kipindi cha pili, Salzburg ambao ni miamba wa soka ya Austria, sasa hawana ushindi wowote katika kampeni za UEFA hadi kufikia sasa msimu huu na wanavuta mkia wa Kundi A.

Atletico ya kocha Diego Simeone iliambulia sare tasa katika mchuano mwingine wa Kundi A uliowakutabnisha na Lokomotiv Moscow nchini Uhispania. Bayern kwa sasa wanaselelea kileleni mwa jedwali kwa alama 12, saba mbele ya Atletico. Lokomotiv wanashikilia nafasi ya tatu kwa alama tatu, mbili zaidi kuliko Salzburg.

You can share this post!

Jinsi mafuriko yanavyoathiri shule zilizoko katika mitaa ya...

KCB yalenga kutikisa msimu mpya kuingia mashindano ya CAF