• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Faith Kipyegon kuacha mbio za mita 1,500 na kuhamia mbio za mita 5,000 baada ya Olimpiki za Tokyo

Faith Kipyegon kuacha mbio za mita 1,500 na kuhamia mbio za mita 5,000 baada ya Olimpiki za Tokyo

Na CHRIS ADUNGO

BINGWA wa Olimpiki katika mbio za mita 1,500, Faith Chepng’etich Kipyegon amefichua azma ya kuanza sasa kunogesha mbio za mita 5,000 baada ya kukamilika kwa Michezo ya Olimpili ya 2021 jijini Tokyo, Japan.

“Maazimio yangu sasa yamebadilika na ninalenga kujitosa kikamilifu katika fani ya mbio za mita 5,000 baada ya kushiriki mita 1,500 kwa mara ya mwisho kwenye Olimpiki zijazo nchini Japan,” akasema Kipyegon.

Hata hivyo, bingwa huyo wa zamani wa dunia katika mbio za mita 1,500 amesema hana maazimio ya kushiriki fani mbili tofauti kwa sambamba jinsi alivyofanya mwanariadha Vivian Cheruiyot aliyetamalaki mbio za mita 5,000 na mita 10,000 kabla ya kuhamia barabarani kwa riadha za masafa marefu.

“Nikiwa mdogo, nilikuwa nikimtazama sana Cheruiyot na nikavutiwa na jinsi alivyofaulu kutamba katika fani mbili tofauti za riadha. Kwa kuwa sasa nina fursa ya kudhihirisha ukubwa wa uwezo wangu katika ngazi nyingine, na ninatarajia makuu,” akasema Kipyegon.

Kipyegon, 26, amejivunia mafanikio tele katika mbio za mita 1,500 – fani ambayo imemzolea dhahabu ya Olimpiki, mataji mengi ya haiba duniani, medali nyingi katika duru za Diamond League, mbio za nyika na mbio za Jumuiya ya Madola mnamo 2014 jijini Glasgow, Scotland.

Kipyegon alijivunia mojawapo ya kampeni bora kwenye ulingo wa riadha mwaka huu wa 2020 baada ya kutoshindwa kwenye mashindano matano tofauti huku akisajili muda bora wa dunia wa dakika 1:57.68 kwenye mbio za mita 800 na dakika 2:29.15 katika mbio za mita 1,000 kwenye duru ya Doha Diamond League nchini Qatar.

  • Tags

You can share this post!

Kampeni za Diamond League msimu ujao kuanzia Rabat, Morocco

TZ yararua Somalia bila huruma Cecafa ikipamba moto