• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 11:34 AM
Raila, Mudavadi kujipima nguvu Matungu

Raila, Mudavadi kujipima nguvu Matungu

VALENTINE OBARA na SHABAN MAKOKHA

KIONGOZI wa Chama cha ODM, Bw Raila Odinga, amepuuzilia mbali wito wa viongozi wa eneo la Magharibi kwamba chama hicho kisiwe na mgombea wakati uchaguzi mdogo utakapoitishwa eneobunge la Matungu, Kaunti ya Kakamega.

Kiti hicho cha ubunge kinatarajiwa kutangazwa wazi hivi karibuni, kufuatia kifo cha mbunge James Murunga ambaye alizikwa Jumamosi.

Katika mazishi hayo, viongozi wa Chama cha ANC walitoa wito pasiwepo na ushindani katika uchaguzi mdogo kwani Bw Murunga alikuwa mwanachama wao.

Seneta wa Kakamega, Bw Cleophas Malala, alimwomba Bw Odinga afuate nyayo za Chama cha Jubilee ambacho kiliamua kutoshindana na ODM katika chaguzi ndogo kadhaa zilizopita tangu 2018, ikiwemo katika eneobunge la Msambweni.

“Tunaomba kiti cha Matungu kiachiwe chama cha ANC,” akasema Bw Malala.

Seneta wa Bungoma, Bw Moses Wetang’ula aliye pia Kiongozi wa Ford Kenya, aliashiria kwamba chama chake hakitakuwa na mgombeaji katika uchaguzi mdogo wa eneo hilo.

Alisema wamefanikiwa kupata umoja na Kiongozi wa ANC Musalia Mudavadi, kwa hivyo anatarajia kutokuwapo ushindani kati yao katika uwaniaji wa ubunge eneo hilo wala Kabuchai, ambako mbunge James Mukwe Lusweti aliaga dunia Ijumaa.

Hata hivyo, Bw Odinga aliposimama kuhutubu alikemea wazo la kutaka kiti hicho kiachiwe ANC huku akikashifu viongozi kwa kuzungumzia suala la urithi wa ubunge kabla Murunga kuzikwa.

“Katika mila yetu hufai kuanza kutamani bibi (wa marehemu) kabla marehemu hajazikwa. Majuzi tulikuwa na uchaguzi Kibra kukawa na wagombeaji wa vyama vingine, na sasa wanasema ODM isiweke mgombeaji hapa. Kwa nini? Sisi tunafuata demokrasia,” akasema.

Tangu Bw Odinga alipoweka mwafaka wa maelewano na Rais Kenyatta almaarufu handisheki, Chama cha Jubilee kimekuwa kikikosa kusimamisha wagombeaji katika chaguzi ndogo kwenye ngome za ODM.

Chama hicho cha Jubilee husema hatua hiyo inanuiwa kutimiza malengo ya handisheki kama vile kuepusha uhasama wa kisiasa.

Hata hivyo, hatua hizo huwa hazipokewi vyema na Naibu Rais William Ruto.

Katika uchaguzi mdogo wa Kibra, Dkt Ruto alimpigia kampeni McDonald Mariga licha ya kuwa viongozi wengine wa chama hicho walisaidia ODM kumpigia debe Bw Imran Okoth.

Katika uchaguzi mdogo wa Msambweni, Dkt Ruto alilalamika alipogundua chama kimeamua hakitakuwa na mgombeaji.

You can share this post!

Watu 18 wafa kwenye mgodi China

UMBEA: Penzi linapochuja, thamani yako pia huwa imechuja