• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Makanisa yasisitiza katiba irekebishwe kubuni uwaziri mkuu

Makanisa yasisitiza katiba irekebishwe kubuni uwaziri mkuu

Na CHARLES WANYORO

BARAZA Kuu la Muungano wa Makanisa nchini (NCCK) limeibua upya wito wa kutaka kufanyia Katiba mabadiliko ili kubuni wadhifa wa waziri mkuu.

Katibu Mkuu wa NCCK Canon Peter Karanja (pichani) alisema kuna haja ya kubuni wadhifa wa waziri mkuu ambaye atakuwa na manaibu wawili pamoja na afisi ya kiongozi wa upinzani atakaye kuwa akilipwa mshahara.

Kasisi huyo alisema kiongozi wa upinzani atakuwa na baraza lake la mawaziri watakaokuwa wakikosoa serikali.

Alisema kuna haja kwa nchi kutumia amani iliyoko nchini, baada ya mwafaka wa ushirikiano baina ya Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa ODM Raila Odinga, kushinikiza mabadiliko ya Katiba ‘ili kuhakikisha amani inadumu.

Akizungumza katika Shule ya Upili ya Moi, Mbiruri katika eneobunge la Runyenjes ambapo alikuwa mgeni rasmi wakati wa hafla ya Siku ya Elimu Askofu Karanja, alisema kubuniwa kwa afisi ya kiongozi wa upinzani pamoja na baraza lake la mawaziri, kutasaidia kuhakikisha kuwa serikali inawahudumia Wakenya kwa uadilifu.

Alisema mfumo wa sasa ambapo mshindi ananyakua kila kitu husababisha mgawanyiko nchini.

“Suala la uchaguzi nchini husababisha mgawanyiko kwa sababu wanasiasa pamoja na wafuasi wao hutumia fedha nyingi katika kampeni. Hivyo, huwa na machungu mwaniaji wao anapopoteza,” akasema.

Alisema kubuniwa kwa afisi ya waziri mkuu na kiongozi wa upinzani kutahakikisha kuwa wawaniaji wenye ushawishi wanaopoteza wanapata nafasi ya kuhudumu.

Kulingana na Askofu Karanja kubuni nyadhifa zaidi serikalini na kutambua rasmi majukumu ya upinzani kutasaidia kumaliza uhasama wa kikabila.

“Kwa sababu Wakenya wote wanataka kuwa serikalini, tunatoa pendekezo kwamba nyadhifa serikalini ziongezwe ili kabila zote ziwakilishwe,” akasema.

“Wadhifa wa Kiongozi wa Upinzani urudishwe na utwaliwe na mwaniaji wa urais anayeibuka nafasi ya pili katika uchaguzi. Tulikuwa na wadhifa huo hapo awali lakini watu wa Mlima Kenya wamekuwa wakisema: ‘kama umeshindwa, enda Bondo. Hii Bondo ambayo utapeleka mtu ambaye ana wafuasi milioni sita, watatoshea wapi?” akauliza.

Askofu Karanja pia aliwataka wanasiasa kukoma kuingilia shughuli za Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) huku akawataka kuunga juhudi zake za tume hiyo katika kurejesha imani ya Wakenya kwake.

You can share this post!

Zaidi ya wanasiasa 10 wagura ODM na KANU, waingia Jubilee

Viongozi Pwani wataka ‘mtu wao’ ateuliwe...

adminleo