• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 3:25 PM
Maafisa wa kaunti waingia mafichoni kuhepa kukamatwa na EACC

Maafisa wa kaunti waingia mafichoni kuhepa kukamatwa na EACC

TOM MATOKE NA BARNABAS BII

 

MAAFISA wakuu katika Serikali ya Kaunti ya Nandi wamekimbilia mafichoni kuhepa maafisa wa Tume ya Ufisadi (EACC) wanaofanya uchunguzi wa sakata ya ubadhirifu wa mabilioni ya pesa katika muda wa miaka mitano iliyopita.

Tume hiyo ya EACC imekita kambi katika kaunti hiyo katika muda wa siku tatu zilizopita huku ikiwasaka maafisa wa sasa na waliokuwepo, wanaohusishwa na pesa hizo kwa kutoa kandarasi za ujenzi wa barabara na pia zabuni bila kufuata utaratibu unaostahili.

Wapelelezi wa tume walifanya misako katika nyumba za maafisa hao katika kaunti za Nandi, Uasin Gishu, Trans Nzoia na Vihiga ambapo walichukua stakabadhi muhimu ambazo ni pamoja na hati miliki za ardhi, mashine za kielektroniki, stakabadhi za zabuni na uagizaji miongoni mwa nyingine.

Afisa mkuu wa polisi eneo la Nandi, Bw Patrick Wambani alithibitisha kuwa kundi la maafisa wa EACC liliomba usaidizi wake kuwasaka baadhi ya waliohusishwa na ubadhirifu wa pesa za umma.

Pia walizuru makao ya aliyekuwa gavana Cleophas Lagat ambapo kaunti wakati wa kipindi chake inashukiwa kupoteza mabilioni kati ya 2014 hadi sasa.

Jumatatu, wapelelezi waliwakamata washukiwa zaidi ya 10 waliohusishwa na uporaji wa pesa za umma miongoni mwao wakiwa ni katibu wa kaunti, Bw Francis ominde na aliyekuwa afisa mwandamizi wa fedha, Bw Emmanuel Wanjala na kuchukua stakabadhi za ardhi na nyingine za zabuni.

Taarifa nyingine zilieleza kuwa maafisa hao walipata kiasi kikubwa cha pesa kutoka kwa afisa wa ngazi za juu baada ya kuvamia nyumbani kwake.

Miongoni mwa waliokamatwa na kuandikisha taarifa katika msako wa EACC ni afisa wa fedha katika kaunti, Bi Helen Katam na aliyekuwa mkuu wa fedha, Bw Charles Muge.

You can share this post!

Ziara za Ruto si tisho kwa ODM – Raila

Walimu wafumaniwa lojing’i wakiwa na wanafunzi

adminleo