• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 1:50 PM
KURUNZI YA PWANI: Thamani ya misitu ya Kaya kwa Mijikenda

KURUNZI YA PWANI: Thamani ya misitu ya Kaya kwa Mijikenda

Na KAZUNGU SAMUEL

MISITU ya kaya katika ukanda wa Pwani ni muhimu sana katika uhifadhi wa mazingira na kuulinda utamaduni.

Katika makabila tisa ya jamii ya Wamijikenda, kila kabila liko na msitu wa kaya ambao hutumika katika shughuli mbalimbali za kitamaduni ikiwemo maombi ya kiasili ambayo yalithaminiwa sana na jamii.

Jamii ya Wamijikenda inashirikisha Wagiriama, Wakauma, Wachonyi, Waribe, Wadigo, Waduruma, Wakambe, Wajibana na Warabai. Kila jamii kati ya hizi inahifadhi msitu wa kaya na kuuthamini katika shughuli za kitamaduni.

Hata hivyo katika miaka ya hivi karibuni,uharibifu wa makaya haya kutokana na uwepo wa shughuli nyingi za kibinadamu umeanza kuzua hali ya sintofahamu.

Zaidi ni hofu ya kuangamia baadaye kwa misitu hiyo endapo hakutakuwa na hatua za haraka zitaazochukuliwa kuhifadhi misiti hii ya kaya.

Mojawapo ya misitu ambayo inakumbwa na hofu ya kuangamia ni ule wa kaya Chonyi ulioko katika kijiji cha Mwarakaya, Vwevwesi, kaunti ya Kilifi. Msitu huo ambao unahifadhiwa na jamii ya Chonyi umeharibiwa sana.

Takribani asilimia sabini ya msitu huo imegeuka kuwa mashamba baada ya wenyeji kuingia ndani na kuanza kufanya shughuli za ukulima.

Hata hivyo katika juhudi za kuhakikisha kwamba misitu hiyo inahifadhiwa, shirika la Umoja wa Mataifa linahohusika na kuhifadhi utamaduni la UNESCO limeanzisha mpango wa kuhakikisha kwamba kaya zote tisa Pwani zinahifadhiwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kile kitakachokuja. UNESCO imeanza mikakati ya kutoa zawadi kwa makaya ambayo yatahifadhi vyema misitu na mazingira yao.

Mwaka jana, msitu wa Kayafungo ulioko katika kaunti ya Kilifi ulitunukiwa kitita cha Sh 750,000 kwa kuibuka kuwa msitu uliotunzwa zaidi.

Msitu huo ni ngome ya jamii ya Wagiriama na unafahamika kwa kulinda mazingira yake dhidi ya uharibifu wa aina yoyote. Msitu huo unapatikana katika kijiji cha Gotani na mbali na fedha, ulipatiwa vifaa vyengine kama vile wilbaro ambazo zitatumika katika kuuhifadhi.

Fedha hizo zilitolewa na tume ya kitaifa ya KNATCOM kwa niaba ya UNESCO ili kuhakikisha kwamba misiti hiyo haiharibiwi tena.

Katika hafla hiyo, ambayo iliongozwa na maafisa wakuu wa KNATCOM akiwemo katibu wa bodi Dkt Evangeline Njoka msitu wa Kaya Gandini/Mtswakara kutoka kaunti ya Kwale uliibuka wa pili. Msitu wa kaya Gandini ulipongezwa kwa kuweka rekodi nzuri kuhusu shughuli zake za kuuhifadhi.

Msitu wa Kaya Chonyi ambao umeharibiwa sana uliibuka nambari ya mwisho na mwito ukatolewa kwa jamii ya Wachonyi kutia bidii ili kuhakikisha kwamba msitu huo hauharibiwi tena.

Mwaka wa 2009, UNESCO ilitoa jumla ya Dola 126,580 za Marekani kwa serikali ya Kenya. Fedha hizo zilitolewa mahsusi kwa ajili ya kuhifadhi misitu ya kaya na vile vile kuhakikisha kwamba maeneo yenye historia za utamaduni yanahifadhiwa.

Pesa hizo zilitolewa kupitia kwa kitengo cha utamaduni katika wizara ya michezo na utamaduni.

Kulingana na Dr Njoka, shirika la KNATCOM linapanga kuangazia juhudi za kuhakikisha kwamba misiti ya kaya inalindwa dhidi ya uharibifu ambao unachochoewa na idadi ya watu ambao wanaingia misituni aidha kulima au kufanya makao.

“Lazima tulinde misiti yetu kwa sababu ndani yake kuna historia ya kale ambayo tutaipoteza endapo tutaiacha ikiangamia,” akasema Dkt Njoka.

Hivi majuzi, mwenyekiti wa Kayafungo Mzee Charo Mlewa aliambia Taifa Leo kuwa wanaendelea na juhudi za kuuhifadhi msitu wa Kayafungo ambao ni maarufu sana katika jamii ya Wagiriama.

“Tangu tuongoze kati ya kaya zote tisa, tumeendelea na juhudi zetu bila kurudi nyuma. Lengo kamili ni kuhakikisha kwamba tunaendelea kuwa bora kwa uhifadhi,” akasema Mzee Mlewa.

Juhudi hizi za kuhifadhi misitu ya kaya pia zimepongezwa na washika dau mbalimbali likiwemo shirika la World Wildlife Fund (WWF) ambalo limekuwa likiongoza juhudi nyingi za kuhifadhi misitu kote nchini.

Akiongea na Taifa Leo afisa wa miradi katika WWF anayesimamia kaunti za Kilifi na Kwale Bw Elias Kimaru, alisema mpango wa KNATCOM kuanza kutoa zawadi kutasaidia pakubwa katika kuhakikisha kwamba misitu inahifadhiwa bila tatizo lolote.

“Mpango huu wa kutoa tuzo kwa misitu bora ya kaya italeta ushindani mkubwa ambao hatimaye utawafanya wazee na jamii ya Wamijikenda kuhifadhi misitu na hili ni jambo la muhimu sana,” akasema Bw Kimaru.

Naye afisa wa misitu katika makavadhi ya kitaifa NMK anayesimamia kaunti ya Kilifi Bw Lawarence Chiro aliponfgeza mpango wa KNATCOM kuanza kutoa tuzo utazifanya jamii ziendelee kuhifadhi misitu bila kuharibu.

You can share this post!

Walimu wanaokwepa kazi kunaswa na BVR

Jombi aaibisha demu aliyetaka warudiane

adminleo