• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 9:50 AM
Wanakijiji waua mamba 300 kulipiza kisasi

Wanakijiji waua mamba 300 kulipiza kisasi

Na MASHIRIKA

JAKARTA, INDONESIA

WANAKIJIJI waliua mamba karibu 300 kulipiza kisasi kwa mwenzao aliyeangamizwa na mmoja wa wanyama hao.

Kulingana na mashirika ya habari, mwanamume alikuwa ameuawa na mamba katika shamba la kuwafuga katika Wilaya ya Sorong, mkoa wa West Papua.

Maafisa wa serikali walinukuliwa kusema mwanamume huyo mwenye umri wa miaka 48 alikuwa akivuna nyasi za kulisha mifugo wakati aliposhambuliwa na kuangamizwa.

Hili halikufurahisha wanakijiji ambao waliamua kulipiza kisasi, wakachukua visu, nyundo na marungu na kuua mamba 292 baada ya kumzika mwenzao.

Picha zilizosambazwa mitandaoni zilionyesha wanakijiji wakiwa wamesimama kando ya mamia ya mizoga ya mamba.

Maafisa wa serikali walisema shamba hilo lilikuwa likifuga mamba tangu mwaka wa 2013 na leseni ilitolewa kwa msingi kuwa ufugaji huo hautatatiza jamii.

Hata hivyo, hatua ya wanakijiji pia ilikashifiwa kwani ilisemekana wangetafuta njia mbadala ya kupooza hasira zao.

-Imekusanywa na Valentine Obara

You can share this post!

Watoto 5 wabambwa kwa kubaka msichana kwa zamu

Kizimbani kwa kuiba TV watazame Kombe la Dunia

adminleo