• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 9:40 PM
Sukari sasa ni salama, Munya aambia Wakenya

Sukari sasa ni salama, Munya aambia Wakenya

Na CECIL ODONGO

WAKENYA hawafai kuhofia kuhusu uwepo wa sukari ghushi sokoni baada ya ripoti ya uchunguzi uliofanywa na maabara ya serikali na Shirika la Kukadiria Ubora wa Bidhaa nchini (KEBS) kutaja kwamba kiasi kikubwa cha sukari iliyonaswa kilikuwa ghushi na kitaharibiwa.

Kulingana na matokeo ya uchunguzi huo, kati ya magunia 1,266,668 ya sukari yaliyoshukiwa kuwa ghushi, magunia 837,224 yalipatikana kuwa hayafai kwa watumiaji bidhaa huku magunia 157,392 yakipatikana kuwa hayana kasoro.

Katika kaunti 28 ambazo sampuli 82 za sukari hiyo zilipimwa, sampuli 31 (38%) zilipatikana na kasoro huku sampuli nyingine 51(62%) zikipatikana kuwa sawa kwa matumizi ya binadamu.

Hata hivyo, kinaya kikubwa  ni kwamba sukari hiyo haikuwa na madini ya zaibaki na shaba jinsi ilivyodaiwa na wengi  ila iliharibika baada ya kuhifadhiwa vibaya katika maghala ya kuhifadhi bidhaa.

Katika kikao na wanahabari ofisini mwake wakati wa kutoa  matokeo hayo, Waziri wa Viwanda Peter Munya aliliagiza shirika linalopigana na bidhaa ghushi nchini liharibu sukari hiyo mara moja  katika shughuli ya wazi  kwa umma na wanahabari.

“Kutokana na matokeo haya, KEBS kwa ushirikiano na taasisi husika zitaharibu kulingana na sheria sukari yote iliyofeli vipimo vya uchunguzi  na walioiagiza watalazimika kugharamia uharibifu huo la sivyo tutaisafirisha katika nchi ilikotolewa,” akasema Bw Munya.

Bw Munya pia alisisitiza kwamba bidhaa zinazoingizwa hapa nchini zitakagukuliwa na ziwekewe alama spesheli ya KEBS ya kuzitambuai kabla hazijaidhinishwa kuuzwa sokoni kama njia ya kuhakikisha ubora wao.

“Tutashiriki ukaguzi wa kipekee kwa mashehena mbalimbali haswa ya bidhaa za vyakula. Pia tutaingia sokoni ili kuondoa  bidhaa ambazo hazijatimiza ubora unahitajika na shirika la KEBS,” akaongeza Bw Munya.

Uchunguzi huo pia ulifichua kwamba,  Kati ya tani 7,750 za sukari zilizonaswa tani 3,555  hazikuwa ghushi na zimerejeshewa wafanyabiashara waagizaji huku KEBS ikiendelea kufanyia uchunguzi tani 4200 zilizosalia.

Waziri huyo pia alithibitisha kwamba serikali imefanyia uchunguzi sampuli 40 ya shehena za mafuta yaliyonaswa  kwa kushukiwa kuingizwa  nchini kimagendo.

Matokeo ya uchunguzi huo yalionyesha kwamba ni shehena 25 ndizo zilifeli vipimo vya KEBS huku 15 zikipatikana kuwa sawa.

You can share this post!

Kizimbani kwa kuiba TV watazame Kombe la Dunia

Magunia ya bangi yanaswa Nakuru

adminleo