• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 7:25 PM
Mibabe wa siasa wajipanga kisiri kuhusu 2022

Mibabe wa siasa wajipanga kisiri kuhusu 2022

Na BENSON MATHEKA

MIKUTANO ya siri kati ya viongozi wakuu wa kisiasa imeshika kasi huku mabadiliko makubwa yakitarajiwa kuhusiana na uchaguzi wa 2022.

Inakisiwa kuwa lengo la mikutano hiyo ni kusuka miungano mipya ya kisiasa, ambayo wadadisi wanasema itaamua mwelekeo wa siasa za Kenya.

Rais Uhuru Kenyatta amekuwa akitutana na kiongozi wa upinzani Raila Odinga, jambo ambalo limewatia tumbojoto washirika wa kisiasa wa Naibu Rais William Ruto.

Mkutano wao wa hivi punde umeripotiwa kufanyika mjini Mombasa. Walipotangaza muafaka wao Machi 29, viongozi hao walikiri kwamba walikuwa wakikutana kwa siri hadi walipokubaliana kufanya kazi pamoja.

Baada ya kukutana Mombasa, Rais Kenyatta alikutana na Rais Mstaafu Daniel Moi na mwanawe Seneta Gedion Moi, nyumbani kwa Mzee Moi, Kabarak.

Rais alisema alipitia kumjulia hali Mzee Moi ambaye ni mlezi wake kisiasa, akielekea katika mazishi ya mke wa jirani yake, Luteni Jenerali Jackson Kasaon.

Hata hivyo, kukosekana kwa Naibu wake William Ruto, hasimu wa kisiasa wa familia ya Moi, ambaye pia alihudhuria mazishi hayo, kulizua maswali kuhusu dhamira ya mkutano huo.

Ikizingatiwa kuwa ziara ya Rais huchukua muda na rasilmali kupanga, wadadisi wanasema haukuwa mkutano wa kupitia tu.

Haikuwa mara ya kwanza Rais Kenyatta kutembelea Mzee Moi akiwa na mwanawe Gedion, ambaye ilisemekana alimzuia Bw Ruto kumuona baba yake alipomtembelea mapema mwaka huu.

Juhudi za Bw Ruto kumtembelea Mzee Moi zilijiri siku chache baada ya Bw Odinga kumtembelea rais huyo wa pili wa Kenya akiandamana na Gedion.

Hii ilifuatiwa na mkutano wa Seneta Moi na wafanyabiashara mabwenyenye kutoka ngome ya kisiasa ya Rais Kenyatta ya eneo la Mlima Kenya.

Duru zilisema kuwa mkutano huo ulilenga kupanga mikakati ya kumjenga Gideon kabla ya 2022 ili aweze kutekeleza wajibu mkubwa.

Wafanyabiashara hao wana ushawishi mkubwa wa kisiasa eneo hilo na Kenya kwa jumla na wadadisi wanasema mkutano wao na Seneta Moi hauwezi kupuuzwa.

Baada ya mkutano huo, mbunge wa Tiaty, William Kamket alinukuliwa akisema kuwa marafiki wote wa Moi ambao wanajali nchi hii wanakutana kote nchini.

Katibu Mkuu wa Kanu, Nick Salat naye alinukuliwa akisema kuwa watu wengi wako tayari kushirikiana na cha Kanu. “Watu wengi wako tayari kuungana nasi kwenye safari hii na tunakutana nao kubadilishana maoni, Tegea tu na hivi karibuni utaona mabadiliko makubwa,” alisema Bw salat.

Kwa upande wake, Bw Odinga amekuwa akikutana na vinara wenzake wawili katika NASA, Kalonzo Musyoka na Musalia Mudavadi kwenye juhudi za kufufua muungano huo.

Tayari, Bw Musyoka, ambaye pia amekutana na Seneta Moi ameongoza chama chake kutangaza kitaunga mkono serikali ya Rais Kenyatta.

Duru zingine zinaeleza kuwa Bw Musyoka, Bw Mudavadi na kinara mwenzao katika NASA Moses Wetangula nao wamekuwa wakikutana bila Raila kupanga mikakati yao ya kisiasa.

Naye Bw Mudavadi na Bw Wetangula wamekuwa wakikutana kuandaa mikakati ya kuunganisha vyao vya ANC na Ford Kenya.

Japo Bw Ruto amekuwa akiendeleza siasa zake za 2022 chini kwa chini, wadadisi wanasema amekuwa akipanga mikakati yake kwa kutuma wandani wake wa kisiasa kukutana na wanasiasa maarufu kote nchini kwa sababu hataki kuonekana kuhujumu serikali ya Jubilee kwa wakati huu.

Baadhi ya wanasiasa tayari wametangaza kuwa watamuunga mkono kwenye uchaguzi wa 2022.

You can share this post!

Warembo wa Uganda wapiga magoti kumshukuru hakimu baada ya...

Matatu ya abiria 14 yanaswa ikibeba wanafunzi 31, wasichana...

adminleo