• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:33 AM
TAHARIRI: Tusikubali madereva watumalizie watoto

TAHARIRI: Tusikubali madereva watumalizie watoto

NA MHARIRI

WANASEMA ajali haina kinga wala kafara, lakini kuna ajali ambazo zinaweza kuzuiwa kama tungekuwa makini na kuzingatia sheria.

Wakati aliyekuwa waziri wa Elimu, Dkt Fred Matiangí alipoagiza mabasi ya shule yawe na rangi ya manjano, hekima iliyokuwepo ni kwamba wananchi wangeweza kutambua kwa urahisi magari hayo.

Wananchi wangejua kuwa mabasi yanabeba wanafunzi, na kwa hivyo wangelikuwa jicho la serikali kuhakikisha madereva hawakiuki kanuni za uchukuzi. Miongoni mwa kanuni hizo ni kupiga marufuku safari za usiku za magari ya kubeba wanafunzi.

Inasahangaza kwamba basi lililowabeba wanafunzi 50 wa wa Shule ya Msingi ya St Gabriel’s Mwingi lilihusika kwenye ajali mwendo was aa sita za usiku. Ikizingatiwa kuwa basi hilo lilitoka Mombasa asubuhi, ina maana kuwa dereva alikiuka kanuni na kuendelea na safari hata baada ya muda unaoruhusiwa.

Isitoshe, dereva wa trela lililokwaruza basi hilo ubavuni na kuliangusha kwenye mto Kanginga, alijawa na ubinafsi na kuamua kulipita basi kwenye daraja.

Kanuni za udereva ziko wazi – kwamba yeyote anayeendesha gari, pikipiki au hata baiskeli, haruhusiwi kumpita mwenzake wanayeelekea upande mmoja iwapo; kuna ukungu na mtu hawezi kuona vyema, kuna kona, kwenye daraja, penye mteremko au mlima na kadhalika.

Kwa kulipita basi kwenye daraja jembamba, inaonyesha dereva wa trela alikuwa na nia ya kukiuka kanuni zote za udereva kwa kuwa alikuwa maeneo ya mashambani.

Kutoroka baada ya ajali hiyo, kunatia hasira kwamba mtu anaweza kugonga gari lenye watoto bila ya kujali maisha ya watoto hao.

Ajali ya jana ambayo tukienda mitamboni ilikuwa imeua watoto 11, inatupatia tahadhari Wakenya tuwe macho na kuwazuia madereva wasiojali kuwaua watoto wetu.

Likizo hii ndio wakati ambapo shule mbalimbali hufanya ziara za masomo katika kila pembe ya nchi. Je, ina maana kuwa watoto wetu wataendelea kufa barabarani eti kwa sababu kuna madereva wasiozingatia sheria? Je, madereva hao wataachwa tu waue wanavyotaka kwa kuwa hakuna mwenye akili timamu anayeweza kuwazuia?

Basi hilo la wanafunzi lilivuka vizuizi vingi barabarani kabla ya ajali hiyo. Hivi polisi wa trafiki wanafahamu kwamba kuna sheria inayokataza mabasi ya shule kusafiri usiku?

Walichukua hatua gani? Pole za wanasiasa na maonyo yao ni muhimu, lakini yafaa tuwe na mfumo unaojisimamia, usiosubiri ajali itokee ndipo kufanywe msako.

You can share this post!

KURUNZI YA PWANI: Kampeni ya kuangamiza unywaji wa pombe...

OBARA: Twahitaji muujiza wa pili ili mwafaka ufanikiwe

adminleo