• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 8:55 PM
Dereva wa lori lililoua wanafunzi 10 akana mashtaka

Dereva wa lori lililoua wanafunzi 10 akana mashtaka

BONIFACE MWANIKI na KITAVI MUTUA

DEREVA wa lori lililosababisha ajali iliyoua wanafunzi 10 wa Shule ya msingi ya Mt. Gabriel mjini Mwingi, Jumatatu alifunguliwa mashtaka tisa ya kusababisha kifo kwa uendeshaji mbaya wa gari.

Abdalla Hassan ndiye aliyekuwa akiendesha lori lilipogongana na gari la shule ya upili ya Nguutani, waliokuwa wametoka ziara ya kimasomo mjini Mombasa.

Hassan alikana mashtaka hayo mbele ya Hakimu Mkuu wa Mwingi, Kibet Sambu, na akaachiliwa kwa dhamana ya Sh5 milioni na mdhamini sawa na kiasi kama hicho.

Kesi hiyo itasikizwa Agosti 20, 2018.

Kwingineko, wanafunzi watatu na mlezi wao jana walikuwa wakitibiwa katika hospitali ya Mwingi Level Five.

Msimamisi wa Matibabu katika hospitali hiyo, Dkt Evans Mumo, alisema hali za wanafunzi hao zimeimarika, ingawa bado wanahitaji kufuatiliwa kiafya kwa karibu.

Wawili kati yao walipelekwa katika chumba cha upasuaji ili kurekebisha miguu yao iliyovunjika, huku wa tatu akipangiwa kufanyiwa upasuaji maalumu. Atafanywa upasuaji huo na madaktari wa Cuba ambao walitumwa kuhudumu katika Kaunti ya Kitui.

“Wanafunzi hao hawamo hatarini, ingawa bado wamelazwa katika wadi zetu. Wamefanyiwa matibabu maalum ili kurekebisha hali zao, hasa miguu yao iliyovunjika,” akasema Dkt Mumo.

Hospitali hiyo pia inajitayarisha kufanya upasuaji kwa miili ya wanafunzi wanane ambao walifariki papo hapo kwenye ajali hiyo. Mwili wa mwanafunzi aliyefariki katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta na mwili wake kurudishwa Mwingi pia utafanyiwa upasuaji.

Waziri wa Afya katika kaunti hiyo Dkt Richard Muthoka alisema upasuaji huo utasaidia katika utambuzi wa miili hiyo kabla ya kukabidhiwa kwa wazazi.

Waziri alisema kaunti hiyo iliwaondolea gharama zote, zikiwemo ada za mochari na upasuaji. Serikali pia itawasaidia katika mipango ya mazishi.

Mkuu wa Dayosisi ya Katoliki ya Kituo Kaasisi Joseph Mwongela alisema kanisa hilo litafanya misa ya wafu kesho kwa wanafunzi 10 ambao walifariki katika ajali hiyo.

“Tumeanza mipango ya mazishi, ambapo kanisa, shule na wadau wengine watakusanyika shuleni kwa maombi maalum baada ya hospitali kumaliza upasuaji na utambuzi wa miili kumalizika,” akasema kasisi huyo.

You can share this post!

Mshauri wa Raila, Silas Jakakimba asakwa Zimbabwe kwa...

Kimombo kilimpiga chenga mfanyakazi wetu, Chandarana...

adminleo