• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 8:31 PM
Kimombo kilimpiga chenga mfanyakazi wetu, Chandarana yajitetea

Kimombo kilimpiga chenga mfanyakazi wetu, Chandarana yajitetea

Na BRIAN OKINDA

WAMILIKI wa maduka ya Chandarana Foodplus yanayokabiliwa na madai ya kueneza chuki na ubaguzi wa rangi wanadai mfanyikazi aliyeandika baruapepe ya kubagua Wakenya, Rima Patel, hajulikani aliko.

Duka hilo pia limelaumu idara inayodhibiti mawasiliano na taarifa zinazotolewa kwa umma kwa kashfa hiyo.

Meneja Msimamizi wa Duka hilo Hanif Rajan aliyekuwa akihojiwa na Tume ya Utangamano (NCIC), alishikilia kuwa mfanyakazi huyo aliajiriwa hivi majuzi na hakuwa na ufahamu wa kutosha wa lugha ya Kiingereza.

“Kufikia sasa hatujui alipoenda kwani alitoweka mara tu baada ya kuandika baruapepe iliyoshutumiwa kote nchini. Hajafika kazini tangu Julai 27 aliposikia kwamba tulilenga kumwadhibu,” akasema Bw Rajan.

Meneja huyo alisema Bi Patel alitoka India na alikuwa amepewa kandarasi ya kufanyia kazi duka hilo kwa kipindi cha miezi mitatu na mkataba ulifikia kikomo Agosti 6.

“Tumetoa taarifa kumhusu kwa maafisa wa uchunguzi ili waweze kubaini alipo,” akasema.

Mkurugenzi wa Idara ya Malalamishi na Masuala ya Sheria wa NCIC, Kyalo Mwengi, alisema tume hiyo imeanzisha uchunguzi ili kubaini kiini cha baruapepe ya ubaguzi wa rangi ambayo iliwakera Wakenya.

“Huku tukiendelea kumsaka mfanyakazi huyo, tunafanya uchunguzi pia kubaini ikiwa ni sera ya duka hilo kuwatunuku wateja kwa misingi ya rangi yao,” akasema Bw Mwengi.

Matokeo ya uchunguzi wa tume hiyo ndiyo yataamua ikiwa mfanyakazi huyo alikiuka sheria au alikuwa mfichuzi aliyeweka wazi uozo wa duka hilo.

You can share this post!

Dereva wa lori lililoua wanafunzi 10 akana mashtaka

Atwoli akana kutoroka na mke wa watu

adminleo