• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Masaibu ya Sofapaka yaipa Gor ushindi, ubingwa wanukia

Masaibu ya Sofapaka yaipa Gor ushindi, ubingwa wanukia

NA CECIL ODONGO

NYOTA ya jaha ilirejea na kumulika kambi ya Mabingwa mara 16 wa KPL Gor Mahia  baada ya kuwalaza mabingwa  wa mwaka wa 2009, Sofapaka mabao 3-0 katika mechi ya KPL iliyosakatwa Agosti 22 kwenye uga wa Narok.

Mabingwa hao walifunga mabao yao kupitia kiungo Joakim Onyango katika dakika ya 33 kisha beki wa kushoto Innocent Wafula akatia msumari moto kwenye kidonda cha Sofapaka kwa kuyafunga mabao mawili safi yaliyozamisha kabisa chombo cha wapinzani katika dakika ya 63 na 84 kipindi cha pili.

Bao la pili la K’Ogalo lilifungwa kupitia penalti baada ya kipa wa Sofapaka Wycliffe Kasaya kumchezea rafu mshambulizi wa Gor Lawrence Juma kwenye boksi.

Kosa hilo liliwaponza mabingwa hao wa zamani kwa kuwa Kasaya alipokezwa kadi nyekundu na ikawalazimu Sofapaka kumaliza mechi wakiwa watu tisa uwanjani.

Masaibu zaidi yaliandama Sofapaka dakika ya 15 baada ya kocha John Baraza  kumwingiza kipa Mathias Kigonya na kumwondoa kiungo  Justin Mico.

Mlinzi Mohamed Kilime aligongana na mlinzi wa Gor Mahia Samuel Onyango na kushindwa kuendelea na mechi dakika kumi za mwisho wa mtanange huo.

Vijana wa Kocha Dylan Kerr sasa wamefungua mwanya wa alama 20 na wanahitaji sare ya aina yoyote katika mechi zao  zilizosalia ili kutwaa ubingwa wa KPL kwa mwaka wa pili mfululizo.

Ushindi huo unawapa matumaini mashabiki wa K’Ogalo ambao  walikuwa wakiendelea kuomboleza kichapo cha Jumapili Agosti 19 mikononi mwa mibabe wa soka ya Rwanda, Rayon Sports kwenye mechi ya kuwania ubingwa wa Kombe la Mashirikisho barani Afrika, CAF.

K’Ogalo sasa watalazimika kurejelea mazoezi kabambe siku ya Alhamisi na Ijumaa kuyanoa makali yao dhidi ya mechi kubwa ya debi ya Mashemeji itakayowakutanisha na watani wao wa jadi AFC Leopards  Jumamosi Agosti 25 katika uga wa MISC, Kasarani kuanzia saa tisa jioni.

Sofapaka walilazimika kumaliza mechi hiyo wakiwa wachezaji kumi

Kichapo hicho sasa kinazima kabisa azma ya Sofapaka ya kuwa wagombezi halisi wa ubingwa wa KPL  msimu wa 2017/18. Batoto ba Mungu wanaonolewa na kocha John Baraza wanaendelea kushikilia nafasi ya nne kwenye msimamo wa jedwali la ligi kwa alama 44 baada ya kujibwaga uwanjani mara 27.

Kocha Dylan Kerr alifanya mabadiliko kadhaa kwa kikosi kilichoicharaza Sofapaka ikiwemo  kumpumzisha kipa Shaban Odhoji na kumtumia Fredrick Odhiambo katika nafasi yake.

Mnyakaji huyo alidhihirisha umahiri wake na kuwanusuru  vijana wa K’Ogalo dhidi ya kufungwa goli la mapema alipookoa penalti iliyozawidiwa Sofapaka na kuchanjwa na mshambulizi matata Kepha Aswani.

You can share this post!

Google sasa yawezesha watumiaji kutuma baruapepe za siri

EACC yaagizwa impe Kidero nakala za ushahidi

adminleo