Kimataifa

AMANI CAR: Wanamgambo watoa masharti 97 kwa AU

August 23rd, 2018 2 min read

MASHIRIKA NA PETER MBURU

VIKOSI vya wanamgambo wa kivita Jamhuri ya Kati mwa Afrika (CAR) vimetoa matakwa 97 kwa Umoja wa Afrika (AU), wakati huu inapofanya juhudi za kuleta amani nchi hiyo ili vikubali kufika meza ya maelewano, zimesema ripoti kutoka AFP.

Kulingana na stakabadhi zinazomilikiwa na AU, matakwa 97 yameorodheshwa na vikosi hivyo, ili kukubali kuweka amani, yakiwemo kuundwa kwa serikali ya muungano.

Vikosi hivyo aidha vinataka msamaha rasmi kwa makosa vilivyotenda na kufanywa mabadiliko katika jeshi la nchi hiyo, ili kukubali kuweka amani.

Muungano wa AU umekuwa ukiongoza juhudi za kurejesha amani nchi hiyo, japo hakujakuwa na hatua ulizopiga.

Nchi hiyo iliingia kwenye vita tangu 2013 baada ya kubanduliwa kwa Rais Francois Bozize (aliyeungwa mkono na wakristo) na kikundi cha muungano wa waislamu kiitwacho Seleka.

Baada ya hapo, wakristo ambao ni asilimia 80 ya taifa hilo waliunda vikundi vya kujiteta na kuviita ‘anti-balaka’.

Nchi ya Ufaransa iliingilia kati kujaribu kulazmu Seleka kuondoka uongozini, kabla ya kupokeza juhudi za kurejesha amani humo muungano wa Umoja wa Mataifa (UN).

Hata hivyo, serikali kuu imekuwa hafifu zaidi, huku ikisalia na udhibiti wa eneo la Bangui pekee, huku vita siku nenda siku rudi vikisababisha vifo vya maelfu wa raia.

Kulingana na afisa aliye eneo la Bangui, wawakilishi wa vikosi hivyo wanatarajiwa kufanya mkutano na timu ya AU katika mji wa Bouar Jumatau kwa nia ya kuoanisha matakwa yao kabla ya kuwasilisha orodha ya mwisho kwa mamlaka.

Lakini serikali hadi sasa imekataa matakwa ya vikosi hivyo.

Russia pia imekuwa sehemu ya kutafuta amani nchi hiyo na inasemekana inaandaa mkutano wa kutafuta suluhu Jumamosi katika jiji kuu la Sudan, Khartoum, kupitia maafisa wa kidiplomasia kutoka Moscow ambao wamekuwa nchi hiyo.

Hata hivyo, msemaji wa CAR Ange-Maxime Kazangui Jumatatu alipinga kuwa serikali yake imehusika katika mazungumzo hayo, akishikilia kuwa wanaunga mkono juhudi za AU.

Kumekuwa na majaribio kadhaa ya kutatua mizozo CAR tangu kuanza kwa vitaa hivyo na maelewano saba ya amani yamewahi kuafikiwa, japo yote hayakuzaa matunda.