Dimba

Arsenal wakemea kunyimwa penalti ‘halali’ dhidi ya Atletico gozi la UEFA

Na MASHIRIKA April 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KOCHA wa Arsenal Mikel Arteta alikemea hatua ya refa ya kubadilisha uamuzi wake wa kuipa timu hiyo penalti kwenye mechi ya mkondo wa kwanza ya nusu fainali ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) dhidi ya Atletico Madrid mnamo Jumatano usiku.

Baada ya kuangalia VAR, Refa Danny Makkelie, alibadilisha uamuzi wake wa kuipa Arsenal mkwaju wa penalti baada ya Eze Eberechi kukanyagwa na Koke.

Mechi hiyo iliyogaragazwa uga wa Metropolitano iliishia sare ya 1-1 na sasa timu hizo bado zina nafasi ya kufuzu fainali katika kipute cha marudiano Jumanne ijayo.

Arteta alidai kuwa Eze alikanyagwa na hoja kuwa refa aliangalia tukio hilo kwenye VAR mara kadhaa ilikuwa ishara tosha kuwa Arsenal walistahili kutunukiwa penalti hiyo.

“Kinachoudhi ni jinsi penalti ya Eberechi ilivyobatilishwa kwa sababu iwapo lazima uiangalie mara 13 ndipo uamue basi ni tukio la ukweli. Pengine hilo goli lingebadilisha kila kitu na tufuzu fainali,” akasema Arteta akionekana kukasirika.

Kocha huyo alisema alikubali penalti ambayo Atletico walipewa baada ya mpira kudunda na kugusa mkono wa Ben White ingawa ingekuwa katika Ligi Kuu Uingereza (EPL) hawangeipata.

Julian Alvarez alifungia Atletico penalti ya Ben White dakika ya 56 na kusawazisha bao ambalo Arsenal walifunga pia kupitia penalti kipindi cha kwanza.

Viktror Gyokeres alifunga penalti baada ya kusukumwa na kuangushwa na David Hancko ndani ya kijisanduku dakika ya 44.

Gyokeres, mvamizi raia wa Uswidi, alifunga penalti hiyo kwa ustadi mno, Kipa Jan Black akiokota hewa.

“Vile tu tulikubali penalti ya Ben White, ni wazi kisa cha Eze kilikuwa penalti,” akaongeza Arteta.

Licha ya ghadhabu hizo, kocha huyo alieleza kuridhishwa kwake na jinsi vijana wake walivyocheza, akieleza imani yake kuwa watafuzu fainali wakipangia vyema Atletico ugani Emirates wiki ijayo.

Atletico walitawala mchezo huo na wangeongeza bao jingine kipindi cha pili lakini shuti ya Antoine Griezman ikagongwa mtambapanya dakika ya 63.

Akizungumza baada ya mechi hiyo, Griezman aliwataka wenzake wajitume na wacheze ugani Emirates jinsi walivyofanya katika kipindi cha pili ugani Metropolitano.

“Mechi ya mkondo wa pili itakuwa ngumu kwa timu zote lakini tukicheza tulivyofanya kipindi cha pili, basi tutatamba. Huo ndio utamu wa soka na jinsi ilivyo kwa sasa, timu yoyote inaweza kutinga fainali,” akasema Griezman kiungo wa Ufaransa.