Dimba

Hatimaye KBC kupeperusha kindumbwendumbwe cha Kombe la Dunia

Na VICTOR OTIENO June 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HOFU miongoni mwa mashabiki wa Kenya kukosa kutazama mechi za Kombe la Dunia sasa haipo tena.

Hii ni baada ya Serikali kutoa fedha zitakazowezesha runinga ya KBC kupata haki za kupeperusha matangazo ya Kombe la Dunia la 2026.

Makala ya 23 ya mashindano hayo makubwa zaidi duniani yataandaliwa kwa pamoja na Amerika, Canada na Mexico.

Kindumbwendumbwe hicho cha siku 39, kitakachoshirikisha mataifa 48, kitaanza Juni 11 yaani Alhamisi ijayo.

Waziri wa Fedha, John Mbadi, alisema jana kwamba serikali imeondoa wasiwasi uliokuwa umezingira suala la KBC kurusha matangazo ya mashindano hayo nchini, kama ilivyozoeleka hapo awali.

Alisema kuchelewa kuthibitishwa kwa KBC kama mtangazaji wa mashindano hayo kulitokana na changamoto za kifedha.

“Nafahamu tulikumbana na changamoto katika kufadhili KBC ili kupeperusha mechi za Kombe la Dunia, lakini sasa tumeziondoa,” alisema Mbadi alipowaalika mabingwa wa Ligi Kuu ya SportPesa, Gor Mahia, katika jengo la Wizara ya Fedha jijini Nairobi.

“Asubuhi ya leo (Alhamisi) nilizungumza na Mkurugenzi Mkuu wa KBC, Agnes Nguna, na kuna jambo analoshughulikia. Tayari tumeidhinisha fedha kutoka kwa serikali kuu kusaidia urushaji wa mashindano hayo,” akaongeza Waziri huyo.

Nguna alithibitisha kuwa KBC itapeperusha mechi za Kombe la Dunia.

“Tunafurahi kuufahamisha umma kwamba Waziri wa Hazina, John Mbadi, kupitia maelekezo maalumu ameidhinisha fedha za kupata haki za matangazo ya moja kwa moja ya bila malipo ili KBC irushe mechi za Kombe la Dunia la FIFA,” alisema Nguna katika taarifa ya habari ya mchana ya KBC.

“Hii ina maana kwamba Wakenya wataweza kutazama mechi hizo mubashara na bila malipo yoyote ya usajili.
Kikosi cha maafisa wetu kwa sasa kinakamilisha makubaliano ya haki hizo na wenye haki za matangazo ili kuhakikisha kila Mkenya anafurahia tamasha hili la kimataifa akiwa nyumbani kwake,” akaongeza.

Kama KBC isingefanikiwa kupata haki hizo za matangazo, mamilioni ya Wakenya wangezuiwa kufuatilia mashindano hayo kwa kuwa upatikanaji wake ungekuwa katika vituo vya runinga vya kulipia pekee.

Kulingana na orodha ya hivi karibuni ya vyombo vya habari ambavyo ni washirika wa FIFA kuhusu Kombe la Dunia, vituo vya runinga vya kulipia vya Azam TV, New World TV na SuperSport International ndivyo pekee vilivyokuwa vimepata haki za kurusha mashindano hayo nchini Kenya.

Hapo awali, Wizara ya Michezo kupitia Mfuko wa Michezo, Sanaa na Maendeleo ya Jamii imekuwa ikiisaidia KBC kwa kutoa fedha za kupata haki hizo za matangazo.

Mnamo Machi 24, Kamati ya Bunge la Kitaifa kuhusu Mawasiliano, Habari na Ubunifu (COIC) ilionya kwamba Wakenya walikuwa katika hatari ya kukosa kutazama Kombe la Dunia kupitia KBC kutokana na ukosefu wa Sh150m zilizohitajika kununua haki hizo.

“Mwenyekiti wa kamati alibaini kuwa KBC inahitaji Sh150m ili kupata haki za matangazo ya bila malipo ya Kombe la Dunia la Shirikisho la Kimataifa la Soka (FIFA) 2026 litakalofanyika Amerika, Canada na Mexico kuanzia Juni 11 hadi Julai 19, 2026,” alisema mwenyekiti wa COIC, John Kiarie, alipowasilisha hoja hiyo kwa Kamati ya Bajeti na Matumizi.

Kanuni za FIFA zinahitaji wapeperushaji wenye haki za kitaifa na wapeperushaji wakuu wa mashindano kurusha idadi fulani ya mechi za Kombe la Dunia kupitia runinga za bila malipo, ingawa idadi hiyo hutofautiana kati ya nchi kulingana na sheria za utangazaji za kila taifa.

Katika Kombe la Dunia la FIFA la mwaka 2022 nchini Qatar, KBC ilifanikiwa kupata haki za kipekee za kurusha mashindano hayo bila malipo nchini Kenya.