Habari

Yafichuka daktari aliyeuawa kwa risasi asubuhi jijini aliwahi kuripoti kupokea vitisho

Na NGINA KIRORI July 31st, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MAUAJI ya mwanasaikolojia Dkt Victoria Nthunya Mutiso kwa kupigwa risasi katika Barabara ya Mbagathi Link, Nairobi, Jumatano asubuhi, yamezua maswali mapya baada ya kubainika alikuwa ameripoti matukio mawili ya kutishiwa maisha miezi michache kabla ya kuuawa.

Sasa maafisa wa Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) wanachunguza iwapo matukio hayo yanahusiana na mauaji yake.

Kwa mujibu wa taarifa za awali za polisi, Dkt Mutiso alikuwa akisafiri kuelekea kazini ndani ya teksi, gari la rangi nyeusi lilipoziba njia katika eneo la Mbagathi.

Mtu aliyekuwa na bunduki alikaribia gari lao na kumpiga risasi kabla ya kutoroka. Wapelelezi wanaamini huenda alifuatwa alipoondoka nyumbani kwake.

Mkurugenzi wa Mawasiliano katika DCI, John Marete, alisema maafisa wa kitengo cha mauaji wanaendelea kukusanya ushahidi wa kisayansi na kurekodi taarifa za mashahidi.

Alisema watu wawili wanaochunguzwa, mwanamume na mwanamke, wanazuiliwa huku uchunguzi ukiendelea.

Mnamo Februari mwaka huu, Dkt Mutiso aliripoti katika Kituo cha Polisi cha Mlolongo kuwa kundi la watu, akiwemo aliowatambua kuwa maafisa wa polisi, walivamia nyumba yake, kuharibu mali na kujaribu kuwaondoa kwa nguvu waliokuwa ndani.

Alidai operesheni hiyo iliongozwa na afisa mmoja mkuu wa polisi. Baadaye alilalamika kuwa hakupatiwa mara moja nambari ya kuripoti tukio hilo (OB), ingawa aliipokea baadaye mwezi Mei.

Kisha Julai 7, aliripoti tukio jingine baada ya mtu aliyekuwa ameabiri pikipiki kushuka akiwa na kitu kilichoonekana kama bunduki na kuelekea kwenye gari lake akiwa amesimama kwenye msongamano wa magari jijini Nairobi.

Aliondoka haraka na kuripoti tukio hilo katika Kituo cha Polisi cha Kilimani.

Wiki tatu baadaye, alipigwa risasi na kuuawa.

Wapelelezi pia wanachunguza iwapo mauaji hayo yanahusiana na mzozo wa muda mrefu kuhusu nyumba aliyokuwa akiishi, ambao ulihusisha kesi kuhusu umiliki na ndoa zilizodumu kwa zaidi ya miaka 20 na hatimaye kusababisha kufurushwa kwa wakazi.

DCI imesema uchunguzi unaendelea kubaini iwapo mizozo hiyo au matukio ya awali yalichangia mauaji hayo.